Beki Hassan Kessy amemvaa Rais wa Klabu ya Simba, Evans Aveva na kumwambia asipotoshe umma na badala yake awaambie ukweli mashabiki na siyo kumtaja yeye ndiyo chanzo cha kukosa ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu.
Hiyo ni siku chache tangu Aveva ataje sababu ya timu hiyo kukosa ubingwa huo uliochukuliwa na Yanga.
Beki huyo, tayari amesaini mkataba wa miaka miwili ya kuichezea Yanga kwa dau la shilingi milioni 40 huku akilipwa mshahara wa shilingi milioni 2 kwa mwezi.
Kessy alisema alichokifanya rais huyo ni kumtumia kama mwamvuli kuwafunika viongozi hao ili wasionekane kikwazo cha wao kushindwa kuiwezesha timu hiyo kutwaa taji hilo.
Kessy alisema kwanza kabisa aliondoka Simba ikiwa timu hiyo imebakiza michezo mingi ambayo kama viongozi na benchi la ufundi wangefanya kazi yake vizuri, ingechukua taji hilo, hivyo anashangaa yeye kutajwa.
Aliongeza kuwa, viongozi hao wasiitumie njia hiyo kumharibia kwa baadhi ya mashabiki wa timu hiyo huku akipanga kwenda kuwavaa mabosi hao akidai malipo yake ya mshahara wa mwezi uliopita baada ya kupata taarifa za malipo hayo.
“Kwanza hao viongozi wa Simba wasijisahaulishe kabisa, wakumbuke ninawadai malipo yangu ya mshahara wa mwezi uliopita, tayari nimeshamwambia katibu wao ninataka mshahara wangu, ni baada kutoona fedha kwenye akaunti yangu.
“Kwa sababu hao viongozi wanajifanya wajanja, bila aibu kabisa wanatangaza kwenye vyombo vya habari kuwa mimi ndiyo sababu ya timu kushindwa kuchukua ubingwa wa ligi kuu, hivi ni kweli hicho walichokiongea!
“Kiukweli kabisa kwanza mashabiki ni mashahidi, mimi niliondoka Simba mapema, baada ya kuona ninatengwa na viongozi, walifungwa mechi na Mwadui FC, nilikuwepo na walipokwenda kucheza na Majimaji na kutoka suluhu nilikuwepo, viongozi hao hawana hoja, ni vema wakawaambia ukweli mashabiki,” alisema Kessy.
Chanzo: Championi

 

Alberto Moreno: Makazi Liverpool, Moyo Sevilla
Gardner Amjibu Lady Jay Dee, agoma kuomba radhi