Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es salaam, inatarajia kuanza kusikiliza maombi ya wadhamini wa aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu ambao wanataka akamatwe ili wajitoe udhamini.

Mahakama imetoa siku 7 kwa upande wa Jamhuri kuwasilisha majibu ya kiapo kinzani na maombi ya wadhamini, Ibrahim Ahmed na Robart Katula Julai 14, mwaka huu.

Wadhamini hao wamefungua maombi wakiiomba itoe hati ya kumkamata kwa kuwa wameshindwa kumpata na kumfikisha Mahakamani hapo.

Maombi hayo namba 2/2020 yalipelekwa mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba ambapo upande wa Jumhuri uliomba kuongezwa muda wa kuwasilisha majibu ya kiapo kinzani.

Hakimu Simba amesema Mahakama itasikiliza maombi hayo Julai 14, mwaka huu na kesi ya msingi itatajwa siku hiyo.

Mbali na Lissu washtakiwa wengine ni Wahariri Simon Mkina, Jabir Idrisa na Mchapishaji wa Kampuni ya Jamana, Ismail Mehbooh.

Katika kesi ya msingi kwa pamoja washtakiwa hao, wanakabiliwa na mashtaka matano ikiwamo kuandika habari za uchochezi kinyume na Sheria ya Magazeti ya Mwaka 2002.

Inadaiwa kati ya Januari 12 na 14, 2016 Dar es salaam, washtakiwa waliandika na kuchapisha taarifa za uchochezi zenye kichwa cha habari ‘Machafuko yaja Zanzibar’

Luc Eymael aweka imani kwa Yikpe
Uchambuzi: Deni la Taifa, maana yake nini?