Baada ya kushinda mataji mawili ya Afrika akiwa na Zambia na Ivory Coast, kocha Mfaransa Herve Renard sasa anaelekea kuweka rekodi nyingine akiwa na Morocco.

Mfaransa huyo ameiwezesha Morocco kuwa timu ya kwanza kufuzu Fainali za Mataifa ya Afrika mwaka 2017, ambazo zitafanyika Gabon.

Mwalimu huyo mwenye umri wa miaka 47 aliipandisha kileleni mwa Kundi F Morocco baada ya ushindi wa 2-0 dhidi ya Cape Verde, mabao ya Youssef El Arabi kipindi cha kwanza mjini Marrakech na kujihakikishia tiketi ya Gabon mwakani.

“Nimefurahishwa na namna ambavyo timu ilicheza vizuri na kuendeleza wimbi la ushindi, tulichokipata ni tulichokitafuta, lakini lazima tutulie na kujiandaa kwa ajili ya fainali,” amesema.

Renard alichukua nafasi ya Badou Zaki katika kikosi cha Morocco ambacho kilikuwa kimepoteza mwelekeo mwezi mmoja uliopita na akaanza na ushindi wa 1-0 dhidi ya Cape Verde.

Kocha huyo anayeamini kuvaa jezi nyeupe ni bahati, alianza kupata umaarufu mwaka 2012 alipoiwezesha Zambia kutwaa taji la AFCON.

Katika mashindano hayo, Chipolopolo iliifunga timu ya Nahodha, Didier Drogba, Ivory Coast kwa penalti baada ya sare ya bila mabao ndani ya dakika 120.

Na mwaka jana Renard, akaiwezesha Ivory Coast kutwaa taji hilo kwa penalti pia baada ya sare ya bila mabao ndani ya dakika 120.

Simba hao wa milima ya Atlasi wameshinda michezo miwili mfululizo nyumbani na ugenini dhdi ya Cape Verde na sasa wanaongoza Kundi F kwa pointi sita zaidi, wakiwa na pointi 12, wakifuatiwa na Cape Verde wenye pointi sita.

Watamenyana na Libya wanaoshika nafasi ya tatu mwezi Juni kabla ya kumalizana Sao Tome e Principe mwezi Septemba.

Ayestaran: Nisingeweza Kuwa Hapa Kama Gary Hakunipendekeza
CCM yaeleza yatoa tamko kuhusu Wabunge wao wanaotuhumiwa Kwa Rushwa