Mwanamfalme, Prince William wa Uingereza anatarajia kukutana na Rais Dk. John Pombe Magufuli wiki ijayo wakati wa ziara yake ya siku saba barani Afrika inayotarajia kuanza Septemba 24 hadi 30, 2018.

Ambapo Katika ziara hiyo ambayo siyo ya kikazi Prince William amelenga kufuatilia juhudi zinazofanywa kukabiliana na ujangili na uhifadhi wa wanyama ambapo atafanya majadiliano na Rais Magufuli, kupigia debe mkutano mkuu wa kukabiliana na ulanguzi wa wanyamapori ambao utaandaliwa jijini London kati ya 11-12 Oktoba na pia atazuru bandari ya Dar es Salaam kujifahamisha zaidi kuhusu juhudi zinazopigwa na taifa hilo.

Mkutano huo ambao kwa kirefu unafahamika kama Illegal Wildlife Trade Conference, unalenga kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika kukabiliana na ulanguzi wa wanyamapori, kwa kuangazia mambo matatu makuu: ulanguzi wa wanyama, wadudu na mimea kama uhalifu, kujenga ushirikiano na kufunga masoko yanayotumiwa na wahalifu kulangua wanyamapori.

Prince William atafanya ziara hiyo akiwa kama Rais wa mashirika yanayotetea uhifadhi wa wanyama ya ‘United for Wildlife na Tusk Trust’ na amekuwa pia mlezi wa shirika la ‘Royal African Society’ linalolenga kukuza uhusiano kati ya Afrika na Uingereza na hushiriki sana juhudi za kukabiliana na ujangili.

Takwimu zinaonesha kuwa Tanzania ilikuwa na tembo 110,000 mwaka 2009 lakini idadi hiyo imeshuka hadi kufikia tembo 43,000 kutokana na ujangili.

Mbali na ziara yake nchini, Prince William anatarajiwa kutembelea pia nchi za  Kenya na Namibia katika ziara hiyo.

Rais Magufuli afanya uteuzi mwingine NSSF
Mbowe: Siwezi kujiuzulu kwa shinikizo la CCM