Kocha Mkuu wa Namungo FC, Thiery Hitimana amesema, mshambuliaji wake tegemeo Blaise Bigirimana huenda akawa sehemu ya kikosi kwenye mchezo wa Fainali Kombe La Shirikisho Tanzania Bara (ASFC) dhidi ya Simba SC.

Mchezo huo utachezwa Agosti 2, mwaka huu kwenye Uwanja wa Nelson Mandela, mjini Sumbawanga.

Bigirimana amesafiri na kikosi cha Namungo FC hadi jijini Mwanza, ambapo leo watacheza dhidi ya Mbao FC na mwishoni mwa juma hili watapambana dhidi ya Alliance FC jijini humo.

Hitimana amesema matarajio ya kumtumia mshambuliaji huyo kutoka nchini Burundi, yamekuja kufuatia hali ya yake kuimarika na huenda akamtumia kwenye michezo ya mwisho ya Ligi Kuu Tanzania Bar.

“Katika mechi za mwisho za ligi tutacheza na Mbao pamoja na Alliance FC, hatuna cha kupoteza ila natumia mechi hizo kuiandaa timu yangu kukabiliana na Simba, tutahakikisha tutakuwa imara kwa ajili ya kutafuta ushindi,” amesema Hitimana.

Kocha huyo amesema anawaheshimu Simba kwa sababu ni timu nzuri na yenye wachezaji wazuri, hivyo analazimika kukijenga imara kikosi chake ili watimize malengo.

“Nina mechi mbili mkononi, sio ngumu kama itakavyokuwa fainali, naifahamu Simba nimekutana nayo, pia juzi nimepata nafasi kuwaona walivyocheza na Alliance, natakiwa kujipanga katika fainali hiyo,” alisema Hitimana.

Namungo FC walitinga Fainali Kombe La Shirikisho kwa kuifunga Sahare All Stars bao moja kwa sifuri Julai 11 mjini Tanga, huku Simba SC wakiisasambua Young Africans mabao manne kwa moja Julai 12 jijini Dar es salaam.

Wachina 2 mbaroni kwa kudukua chanjo ya Corona Marekani
Meneja asimamishwa kazi kwa upotevu wa ng'ome 32