Hofu yatanda miongoni wa baadhi ya wazazi ndugu na jamaa katika kijiji cha Mtimbwilimbwi, mkoani Mtwara baada ya watoto 11 wa kiume, wakiwemo wanafunzi wa shule za msingi na sekondari kutoweka kwa zaidi ya siku 10 sasa.

Imeelezwa kuwa watoto hao ni mara ya pili wanapotea katika mazingira ya kutatanisha, ambapo awali walipotea kwa siku saba na kukamatwa nchini Msumbiji.

Mshamu Mtanda, mmoja kati ya wazazi wa watoto hao ameliambia gazeti la Uhuru kuwa Oktoba 16 mwaka huu alipewa taarifa kuwa mtoto wake Hairu Mshamu ametoweka tangu alipokwenda kucheza.

” Mpaka unafika muda wa mchana hajarudi na nikauliza tena yuko wapi ili tuandae chakula cha mchana tule pamoja, lakini sikupata majibu” alisema mzazi huyo.

Na kueleza kuwa alimsubiri mtoto wake hadi saa 12:00 jioni na hakuona dalili yeyote ya kurudi kwa mtoto huyo ndipo alipolazimika kwenda kumtafuta kwa majirani.

” Nlikwenda kwa jirani yangu nikamuuliza kama amemwona mwanangu, hata hivyo alinijibu naye pia watoto wake wawili hawajulikani walipo tangu asubuhi, ikabidi tuanze kutembea kwa baadhi ya wazazi wengine, kuulizia na jibu lilikuwa lile lile kuwa hawapo” alieleza Mtanda.

Kwa upande wa mzazi mwingine, Moza Thobias, ambaye pia mtoto wake amepotea amesema kuwa yeye mtoto wake hii ni mara ya pili kupotea.

“Mwakajana aliondoka bila taarifa, baada ya siku tatu alikamatwa mpakani mwa Tanzania na Msumbiji kwenye kijiji cha Mpondanyali. Nilipo muuliza alienda wapi na kwanini aliondoka alisema rafiki yao alimpiga mzee kijijini, hivyo wao walianza kutishwa ndio maana wakakimbia” alifafanua Moza.

Akizungumzia tukio hilo, Diwani kata ya Mtimbwilimbwi, Salum Chihipu amesema watoto hao wamepotea katika mazingira ya kutatanisha kwani miongoni mwao walipotea mwakajana.

Amesema tayari wametoa taarifa kituo cha polisi Nanyamba na wameshaanza hatua za awali za kuwaita wazazi na kuzungumza nao.

Mkuu wa wilaya ya Mtwara, Evod Mmanda amesema Serikali ina taarifa hiyo na wamesha wahoji wazazi .

Ameongeza kuwa kwa sasa ni msimu wa korosho na inawezekana wapo kwenye mashamba ya wakulima wakubwa wakiokota korosho na ametoa wito kwa wazazi kuwa karibu na watoto wao hasa kipindi hiki cha msimu wa korosho.

Zahera aendelea kupambana na hali yake
Serikali yakemea ubadhirifu wa dawa