“Ni furaha kucheza dhidi ya timu kubwa na yenye ushindani katika ukanda wa Afrika mashariki na Kati” ni kauli iliyotolewa na Kocha wa Mabingwa wa Soka nchini Sudan Al Hilal Flolent Ibenge.

Ibenge wamewasili jijini Dar es salaam leo Jumatano (Januari 25) sambamba na kikosi cha wachezaji 39 pamoja na baadhi ya maafisa wa klabu hiyo yenye maskani yake katika kitongoji cha Omdurman jijini Khartoum.

Kocha huyo kutoka DR Congo amesema hatua ya kikosi chake kupata nafasi ya kucheza michezo mitatu ya kimataifa ya kirafiki ambayo ni sehemu ya kambi yao ya maandalizi hapa Tanzania, ni bahati kubwa na anaamini itawasaidia kufanya vizuri kwenye mchezo wao wa kwanza Hatua ya Makundi Ligi ya Mabingwa Barani Afrika dhidi ya Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini.

Al Hilal itacheza dhidi ya Namungo FC Januari 26, kisha Januari 31 itapambana na Azam FC, michezo yote hiyo ikichezwa Uwanja wa Azam Complex Chamazi jijini Dar es salaam.

Februari 05 kikosi cha Al Hilal kitashuka dimba na Benjamin Mkapa kupapatuana na Simba SC ambayo ni sehemu ya timu 16 zitakazoshiriki Hatua ya Makundi Ligi ya Mabingwa Barani Afrika msimu huu 2022/23.

Pia Simba SC itautumia mchezo huo wa kimataifa wa kirafiki dhidi ya Al Hilal kujiandaa na mchezo wake wa kwanza wa hatua ya Makundi Ligi ya Mabingwa Barani Afrika dhidi ya Horoya AC utakaopigwa nchini Guinea mapema mwezi Februari.

Simba SC imepangwa Kundi C sambamba na Horoya AC (Guinea), Raja Casablanca (Morocco) pamoja na Vipers SC (Uganda).

Klabu ya Al Hilal imepangwa Kundi B sambamba na Al Ahly (Misri) Mamelodi Sundowns (Afrika Kusini) na Cotton Sports (Cameroon).

Katekista Mahakamani kwa kumbaka Mwanafunzi
Simba SC yamuwinda Kwesi Apiah