Kikosi cha Azam FC kimedharia kuirarua Kagera Sugar katika mchezo wa Mzunguuko wanane wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaochezwa Alhamis (Desemba 09) Uwanja wa Azam Complex Chamazi jijini Dar es salaam.

Azam FC iliyoanza kurejea kwenye makali yake, baada ya kuanza Ligi Kuu msimu huu kwa kusuasua, imeonyesha dhamira hiyo kupitia kwa Mshambuliaji wake kutoka DR Congo Idriss Mbombo.

Mbombo ambaye alifunga bao la ushindi kwenye mchezo uliopita dhidi ya Mtibwa Sugar, amesema wamejipanga kuwamaliza Kagera Sugar kwenye mchezo huo ili kuipa timu yao alama tatu muhimu.

“Kikubwa kuelekea kwenye mchezo wetu maandalizi yapo sawa na tunahitaji kupata alama tatu ili kuweza kuendelea kwenye kasi yetu ambayo tumeanza nayo.”

“Mashabiki wajitokeze kwa wingi kwa kuwa tutakuwa nyumbani na tunachohitaji ni kuona kwamba timu inapata ushindi.” amesema Mbombo

Azam FC imeshajikusanyia alama 10 zinazoiweka katika nafasi ya 7 katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu 2021/22, huku Kagera Sugar ikishika nafasi ya 12 kwenye msimamo huo kwa kufikisha alama 8.

Kabwili kuachwa Dirisha Dogo
Try Again: Tuna timu ya kumfunga yoyote