Licha ya Kuibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya Mabingwa Watetezi Young Africans, Kocha Mkuu wa Ihefu FC Juma Mwambusi ameanza mikakati ya kukiongezea nguvu kikosi chake kupitia Dirisha Dogo la Usajili.

Mwambusi ambaye ameweka Rekodi ya Kipekee msimu huu kwa kuwa Kocha wa kwanza kuifunga Young Africans iliyokua inatamba Rekodi ya kucheza michezo 49 ya Ligi Kuu bila kupoteza, amesema anatarajia kuongeza Wachezaji wawili kwenye usajili wa dirisha dogo kwa lengo la kukiongezea nguvu kikosi chake.

Ihefu iliuanza msimu vibaya, kwani katika michezo 14 ilizocheza hadi sasa kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara, imeshinda mitatu, sare mbili na kupoteza tisa, hivyo kuvuna alama kumi na moja, zinazoiweka katika nafasi ya 13.

Kocha Mwambusi, amesema anahitaji idadi hiyo ya wachezaji ili kuiongezea nguvu safu yake ya ushambuliaji na ambayo imeonekana kuwa na mapungufu msimu huu.

“Safu ya umaliziaji ina mapungufu, mara nyingi washambuliaji wangu wanapata mipira [sehemu sahihi] lakini wanashindwa kufunga, hivyo inanipasa nifanye usajili mzuri,” amesema Mwambusi.

Kocha huyo amesema washambuliaji wake wamekuwa hawatulii kwenye lango lao jambo lililowasababishia kupoteza michezo yao iliyopita.

“Michezo yetu iliyopita hatujafanya vizuri kutokana na upungufu huo, japo timu inajitahidi kucheza ikiwa uwanjani lakini umaliziaji ndio tatizo.”

ASFC: Young Africans, Simba SC zapata wapinzani
Ahmed Ally: Ihefu FC imetufurahisha sana