Rais wa Iran, Hassan Rouhani ameishauri Marekani kurudi katika makubaliano ya mkataba wa nyuklia wa mwaka 2015 uliofikiwa kati ya Iran na mataifa makubwa.

Ameyasema hayo katika kikao cha baraza lake la mawaziri, ambapo ameitaka Marekani kutimiza wajibu wake katika makubaliano hayo kwamba kufanya hivyo, itakuwa njia fupi kabisa ya kutimiza maslahi ya pande zote mbili.

Katika tovuti yake, Rouhani ameionya Marekani dhidi ya kutumia nguvu za kijeshi kwa Iran na kwamba watakapokiuka mipaka ya Iran, basi itachukua hatua stahiki dhidi ya Marekani.

Aidha, mgogoro baina ya Marekani na Iran ulianza mwaka mmoja uliopita baada ya Marekani kujitoa katika makubaliano ya mkataba wa Nyuklia baina yake na Iran na mataifa mengine yaliyo na nguvu duniani na kisha kuanza kuiwekea vikwazo Iran.

Hivi karibuni Iran ilizidisha mara nne utengenezaji wa silaha za Nyuklia kwa lengo la kuvunja mojawapo ya makubaliano ya mkataba huo na kutishia kwamba itaongeza kutengeneza silaha nyingine zilizo na kiwango cha juu cha Uraniam kufikia Julai 7, iwapo mataifa ya Ulaya yaliyotia sahihi mkataba huo hawatatoa makubaliano mengine mapya.

Kiongozi wa kidini wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei amesema Iran kamwe haitabadilisha msimamo wake kwa vikwazo vya Marekani.

“Marekani ni nchi iliyo na uovu mkubwa duniani, imesababisha vita, umwagikaji wa damu na mgawanyiko. imekuwa ikifanya ulanguzi na wizi katika mataifa mengine. Imekuwa hivyo kwa muda mrefu sana, sio kwa miaka kumi ama ishirni iliyopita. Watu wanaochukiwa zaidi katika utawala huo wanaishutumu Iran, siku haipiti bila ya kuilaani ama kuitukana Iran. Hatutarudi nyuma kwa kutulaani na kutudhalilisha,” amesema Khamenei.

Mkuu wa Jeshi la Mapinduzi la Iran, Hossein Salami amesema kuwa vikwazo vya Marekani kwa Iran ni hatua za kukosa matumaini baada ya Iran kutungua ndege yao isiyokuwa na rubani katika ghuba ya Omani.

James Kotei atimkia Kaizer Chiefs
Watumiaji dawa za kulevya wapungua Tanzania