Katika kuhakikisha kuwa tafiti mbalimbali zinazofanywa na Mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali kwa ajili ya maendeleo ya jamii zinafanyiwa kazi, Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Selemani Jafo amewataka watumishi wa umma kutozifungia kabatini.

Jafo amesema kuwa tafiti ambazo zimekuwa zikifanywa na Mashirika mbalimbali ni muhimu sana katika utatuzi wa kero mbalimbali zinazo ikumba jamii.

Ameyasema hayo Mjini Dodoma wakati wa uzinduzi wa ripoti ya sita ya mwaka ya upimaji kujifunza iliyotolewa na Shirika la Twaweza.

“Kumekuwa na tabia mbaya kwa baadhi ya wataalamu wetu wa Serikali, tafiti hizi zinazotolewa na mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali kutokuzifanyia kazi, kwani wengi wao huwa wanazifungia ndani ya makabati,”amesema Jafo.

Aidha, Jafo ameongeza kuwa kuanzia sasa mtaalamu yeyote atakaebainika kutofanyia kazi tafiti hizo kwa kuzifungia kabatini atachukuliwa hatua kali kwani Mashirika mengi yamekuwa yakitumia muda mwingi kwa ajili ya kazi hiyo.

Hata hivyo, Naibu Waziri huyo amesema watayafanyia kazi mapungufu yote yaliyojitokeza katika ripoti hiyo ili yaweze kuwafikia walengwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Twaweza, Aidan Eyakuze amesema kuwa tafiti hizo zinzofanywa na Shirika hilo zinajumuisha nchi mbalimbali barani Afrika.

LIVE: Rais Magufuli katika uzinduzi wa ujenzi wa Reli ya kisasa
Barua yakutwa karibu na basi la Borussia Dortmund lililoshambuliwa kwa milipuko