Vyama vya siasa nchini vimetakiwa kutekeleza majukumu yao ya kisiasa kwa kufuata na kuzingatia sheria na kanuni za vyama vya siasa na si vinginevyo.

Agizo hilo limetolewa na Msajili wa Vyama vya Siasa nchini Tanzania, Jaji Francis Mutungi kufuatia tabia iliyojitokeza  ya baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa nchini kutumia vibaya vyombo vya habari, hususani mitandao ya kijamii kufanya vitendo au kutoa kauli ambazo zinavunja sheria za nchi.

“Ninasisitiza kuwa viongozi wa vyama vya siasa wasitumie vibaya dhana ya demokrasia na uhuru wa habari, kuvunja Sheria za nchi. Ieleweke kwamba mtu yeyote anapokiuka sheria za nchi, Sheria itachukua mkondo wake bila kujali wadhifa wa mhusika katika chama cha siasa, amesema Jaji Mutungi.

Hata hivyo, Jaji Mutungi ametoa rai kwa viongozi wote wa vyama vya siasa na wanachama wote wa vyama vya siasa nchini kuheshimu sheria za nchi wakati wote ili kudumisha na kukuza demokrasia ya vyama vingi nchini.

 

Zari ala shavu shindano la Miss Uganda 2018
Rais wa Zanzibar afanya uteuzi wa wajumbe 6 Tume ya Uchaguzi