Vijana nchini wametakiwa kuienzi na kuendelea kuitunza amani iliyoachwa na waasisi wa taifa ili kuijenga Tanzania yenye amani na utulivu kwa mustakabali wa kizazi cha sasa na baadaye.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dar es Salaam na Waziri Mkuu Mstaafu Jaji Joseph Warioba wakati wa ufunguzi wa Mhadhara wa Tatu wa Mwalimu Nyerere uliojadili maendeleo ya elimu ya juu Afrika ulioambatana na ufunguzi wa hifadhi ya nyaraka ya Mwalimu Nyerere.
Jaji Warioba alisema kuwa vijana wanatakiwa kuenzi na kuendeleza amani iliyoachwa na waasisi wetu kwa kuwa imejenga misingi bora katika kwa vizazi vya Watanzania.
“Vijana ni nguvu kazi ya taifa hivyo mnapaswa kuitunza na kuendeleza amani ambayo imeachwa na waasisi wa taifa kwa maendeleo ya nchi yetu”Alisema Jaji Warioba.
Aidha Warioba aliongeza kuwa vijana waache kutumia muda wao kuzungumzia siasa na badala yake watumie nguvu na akili kufanya maendeleo yao na ya jamii kwa ujumla ili kuijenga nchi.
Kwa mujibu wa Jaji Warioba alisema kuwa vijana wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuimarisha umoja na mshikamano ili kuondokana na ubaguzi wa rangi, kabila, vyama vya siasa na dini na kupigana na maadui watatu wa umasikini, ujinga na maradhi.
Hata hivyo Jaji Warioba aliwataka kuwa wana siasa nchini kuwa msaada mkubwa wa wananchi badala ya wananchi kugeuka msaada kwa wanasiasa.