Mdau wa Soka la Bongo Jemedari Said Kazumari amekosoa maamuzi ya Shirikisho la soka Tanzania ‘TFF’ ya kuruhusu Usajili wa Kiungo Mshambuliaji kutoka DR Congo Tuisila Kisinda kujiunga na Young Africans kama mchezaji wa Kimataifa.

TFF ilizuia usajili wa Kiungo huyo kwa kigezo cha Young Africans kuwa na idadi ya wachezaji 12 wa Kimataifa waliosajiliwa kwa msimu wa 2022/23, lakini jana Alhamis (Septemba 15) majira ya jioni Shirikisho hilo lilithibitisha kuruhusu usajili wa Mchezaji huyo, kufuatia Mshambuliaji Lazarius Kambole kuuzwa nchini Uganda.

Jemedari amepinga maamuzi hayo akiwa katika Kipindi cha Sports HQ cha EFM leo Ijumaa (Septemba 16), akisema maamuzi hayo ya TFF huenda yakatoa msukumo na kuleta usumbufu katika usajili wa misimu inayokuja kwa klabu nyingine za Ligi Kuu ama Young Africans yenyewe.

Amesema TFF ilipaswa kuendelea kusimamia maamuzi iliyoyachukua baada ya kufungwa kwa Dirisha la Usajili, lakini kugeuza na kumruhusu Mchezaji huyo kuingia kwenye usajili wa Young Africans kwa kigezo cha kuuzwa kwa Kambole, imempa mashaka na hofu kwa mustakabali wa usajili wa wachezaji kwa siku za usoni.

“Simchukii mtu, lakini hiki kilichofanyika kwa Kisinda kitakuja kusumbua baadae. Tunakubaliana kuhusu busara, lakini kama busara ilipaswa kufanyika siku ya kwanza ambayo Young Africans waliomba.”
“Kama Young Africans hawakuwa sahihi siku ile ya kwanza, ilipaswa kusimama hivyo hivyo. Lakini kukataa kisha kuja kukubali ni kuleta mkanganyiko” amesema Jemedari

Kisinda ambaye aliwahi kuitumikia Young African msimu wa 2020/21 kabla ya kutimkia RS Berkane ya Morocco, alisajiliwa tena klabuni hapo dakika za mwisho kabla ya kufungwa kwa Dirisha la Usajili mwishoni mwa mwezi Agosti, 2022.

Simba SC yafunguka hatma ya Dejan Georgijevic
Kocha Nabi achimba mkwara Young Africans