Beki wa kati kutoka nchini Kenya na klabu ya Simba SC Joash Achieng Onyango, amekubali kuongeza mkataba wa kuendelea kukipiga ndani ya timu hiyo ya Msimbazi jijini Dar es salaam.

Onyango anatajwa kukubali dili hilo, baada ya siku chache tangu tetesi zizagae za beki huyo tegemeo kunako Simba kugomea mazungumzo ya awali kati yake na uongozi wa timu hiyo.

Onyango ni kati ya wachezaji wanaomaliza mikataba katika kikosi hicho mwishoni mwa msimu huu, wengine baadhi ni Rally Bwalya, Pascal Wawa, Hassan Dilunga, Bernard Morrison na Aishi Manula.

Mmoja wa mabosi wa Simba, amesema tayari uongozi umeanza kufanya mazungumzo na baadhi ya wachezaji ambao kocha mkuu wa timu hiyo, Mhispania, Pablo Franco amewapendekeza waongezewe mikataba.

Bosi huyo amesema kwa kuanza wameanza na Onyango ambaye anatajwa kuwaniwa na baadhi ya klabu za ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kumsajili.

Ameongeza kuwa, uongozi wa timu hiyo, juzi Jumapili mara baada ya mchezo wa ligi dhidi ya Ruvu Shooting, ulimuita na kufanya naye mazungumzo kwa ajili ya kumuongezea mkataba mwingine wa miaka miwili.

“Uongozi umepata taarifa za baadhi ya wachezaji wetu tegemeo ambao wameonesha kiwango kizuri katika michuano ya kimataifa kuhitajika na baadhi ya klabu za ndani na nje ya nchi.

“Hivyo haraka umeanza kufanya nao mazungumzo na kati ya hao yupo Onyango ndiye amekuwa mchezaji wa kwanza kuanza kufanya naye mazungumzo.

“Katika mazungumzo hayo, Onyango ameonekana kukubali kuongeza mkataba mpya kwa makubaliano maalum ikiwemo kuongezewa dau la usajili na mshahara,” alisema bosi huyo.

Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez, amethibitisha hilo kwa kusema: “Tumeanza kufanya mazungumzo na baadhi ya wachezaji ambao mikataba yao inaelekea ukingoni.

“Kati ya hao yupo Onyango ambaye ataendelea kuichezea Simba katika misimu mingine miwili mara baada ya kufikia muafaka mzuri.”

Mwandishi wa Al Jazeera auwawa kwa Risasi kichwani
Young Africans yaachana na Abeid Bigirimana