Nahodha na mshambuliaji wa Azam FC, John Raphael Bocco ‘Adebayor’ amesema wataifunga Yanga SC Jumamosi Uwanja wa Taifa Dar es Salaam katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.

Bocco amesema kwamba wanaijua vizuri Yanga SC na wataifunga Jumamosi.

“Tunawajua Yanga, ni timu nzuri kweli. Lakini sisi tunajua namna ya kuwafunga. Na tutawafunga tu,”amesema.

Bocco amesema kwamba makosa waliyofanya katika mechi mbili zilizopita walizokutana na Yanga SC kumaliza dakika 90 bila kufunga bao, hawawezi kuyarudia.

Mechi mbili za awali msimu huu kuzikutanisha Yanga na Azam FC kila timu ilishinda moja, tena kwa mikwaju ya penalti.

Azam FC ilianza kuifunga Yanga SC kwa penalti 5-3 kufuatia sare ya 0-0 ndani ya dakika 90 katika Robo Fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na kati, Kombe la Kagame Julai mjini Dar es Salaam.

Na Yanga SC ikalipa kisasi kwa ushindi wa penalti 8-7 baada ya sare ya 0-0 ndani ya dakika 90 katika mchezo wa Ngao ya Jamii Uwanja wa Taifa Agosti mwaka huu.

Jumamosi zikikutana kwa mara ya tatu, utakuwa mchezo wa kuwania usukani wa Ligi Kuu na pia kumaliza ubishi wa nani zaidi baina yao.

Kwa ujumla Ligi Kuu inandelea Jumakosi kwa mechi sita kupigwa kwenye viwanja tofauti na mbali na Yanga SC kumenyana na Azam FC Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam- Majimaji FC wataikaribisha African Sports Uwanja wa Majimaji, Songea na Mbeya City watakuwa wenyeji wa Simba SC Uwanja wa Sokoine, Mbeya

Ndanda FC wataikaribisha Toto Africans Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara, Stand United wataikaribisha Prisons Uwanja wa Kambarage, Shinyanga na Coastal Union watakuwa wenyeji wa Mtibwa Sugar Uwanja wa Mkwakwani, Tanga, wakati Jumapili Mgambo Shooting wataikaribisha Kagera Sugar Mkwakwani na Mwadui FC watakuwa wenyeji wa JKT Ruvu Uwanja wa Mwadui Complex.

Lembeli Awapa Neno Wagombea Wa CCM Waliomtangazia ‘Maafa’ Baada Ya Ajali
JK: Taifa Stars Ina Mlima Wa Kupanda