Mshambuliaji kutoka Burkina Faso Jonathan Pitroipa, ametangaza kustaafu soka la kimataifa, baada ya kuitumikia timu ya taifa lake (The Stallions) kwa muda wa miaka 13.

Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 33, ambaye kwa sasa anaitumikia klabu ya Paris FC inayoshiriki ligi daraja la pili Ufaransa, alikua sehemu ya kikosi cha Burkina Faso, kilichotinga hatua ya fainali mwaka 2013, ambacho kilipoteza dhidi ya Nigeria.

Pitroipa alitangazwa kuwa mchezaji bora wa fainali za AFCON kwa mwaka huo, baada ya kuonyesha kiwango kizuri, ambacho kiliisaidia Burkina Faso  kutinga hatua ya fainali.

Miaka minne baadae, bado mshambuliaji huyo alionekana kuwa katika kiwango cha juu, kwa kuisaidia Burkina Faso kuchukua nafasi ya mshindi wa tatu katika fainali za AFCON, zilizounguruma Gabon.

“Ni kweli nimeamua kuchukua maamuzi ya kustaafu soka la kimataifa, ni vigumu kufikia maamuzi haya, lakini imenilazimu kufanya hivyo, ninaamini ni wakati sahihi kwangu kukaa pembeni ili kuwapisha wengine,” aliandia Pitroipa katika ukurasa wake wa Facebook.

“Katika miaka ya karibuni nimekua na uwajibikaji mkubwa katika timu yangu ya taifa, imenichukua muda mwingi kuhakikisha ninafikia hatua ya juu zaidi, ninaamini nilipofikia panatosha, ni zamu ya vijana kuendeleza nipofikia mimi.”

“Sina budi kuwashukuru wachezaji wote niliocheza nao kwenye timu ya taifa, mshabiki, watu wangu wa karibu ambao walikua wakinipa faraja na kunishauri wakati wote, ili kufanikisha furaha ya ushindi, familia yangu nayo ninaishukuru sana.”

“Ninajivunia kuvaa jezi ya timu yangu ya taifa, daima nitaendelea kuikumbuka hatua hiyo ambayo imenifanya kuwa shujaa niliepambana kwa maslahi ya taifa langu, kupitia mchezo wa soka.”

Kwa mara ya mwisho mshambuliaji huyo alionekana akiwa na kikosi cha Burkina Faso wakati wa michezo ya awali ya kuwania kufuzu fainali za Afrika (AFCON 2021) iliyochezwa mwezi uliopita.

Burkina Faso walianza kwa matokeo ya sare ya bila kufungana dhidi ya Uganda, na siku nne baadae walipata ushindi wa mabao mawili kwa moja dhidi ya Sudan Kusini.

Mbwana Samatta atemwa tuzo za Afrika
Kashfa ya kudanganya umri yamng'oa Mwenyekiti UVCCM Mtwara