Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai amemuandikia barua Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji Semistocles Kaijage kumjulisha kuwa jimbo la Arumeru Mashariki lililokuwa likiongozwa na mbunge wa chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Joshua Nassari lipo wazi kutokana na mbunge huyo kupoteza sifa za kuendelea kuwa mbunge.

Katika barua hiyo, imeeleza kuwa mbunge huyo amekosa sifa za kuendelea na ubunge wake kutokana na tabia yake ya kutohudhuria mikutano mitatu ya bunge, ambapo ameitaja kuwa ni mkutano wa Kumi na Mbili wa tarehe 4- 14 Septemba, 2018, Mkutano wa Kumi na Tatu wa tarehe 6- 16 Novemba 2018 na Mkutano wa Kumi na Nne wa tarehe 29 Januari mpaka 9 Februari 2019.

Aidha, barua hiyo imesema kuwa uamuzi huo wa spika umezingatia masharti ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 71(1)(c), ambapo ibara hiyo inaeleza kuwa ”Mbunge atakoma kuwa mbunge na ataacha kiti chake cha ubunge ikiwa ataacha kuhudhuria vikao vya mikutano ya bunge mitatu mfululizo bila ya ruhusa ya Spika”

Ibara hiyo tena imefafanuliwa pia katika kanuni ya 146(1) na (2) za kanuni za kamati ya kudumu za bunge toleo la Januari 2016, ambapo kanuni hiyo inaeleza kuwa, ”Kuhudhuria vikao vya bunge na kamati zake ni wajibu wa mbunge, mbunge yeyote atakayeshindwa kuhudhuria mikutano ya bunge mitatu mfululizo bila ruhusa ya Spika iliyotolewa kwa maandishi atapoteza ubunge wake na Spika ataitaarifu tume ya taifa ya uchaguzi”

Kufuatia taarifa hiyo, Tume ya Uchaguzi inaweza kuitisha uchaguzi ili iweze kumpata mbunge wa kuziba nafasi hiyo,

 

RC Songwe: Fuatilieni wanaouza Pembejeo Feki
Mtangazaji apigwa vibaya na aliojaribu kuwasaidia katika ajali