Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli amewaapisha viongozi watatu aliowateua hivi karibuni na kuwapatia maagizo watakayotakiwa kutekeleza katika majukumu yao waliyoanza rasmi leo.

Viongozi walioapishwa ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. John Kiang’u Jingu, Balozi wa Tanzania nchini Uganda Dkt. Aziz Ponary Mlima na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) CP Diwani Athumani Msuya.

Aidha, Rais Magufuli amemtaka Dkt. Jingu kwa kushirikiana na viongozi wengine wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kufuatilia usajili na utendaji kazi wa mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO’s), na kuhakikisha yanafanya kazi kwa kuzingatia sheria ambazo pamoja na mambo mengine zinawataka kuendesha shughuli zao kwa uwazi hususani masuala ya mapato na matumizi ya fedha za ufadhili wa shughuli zake.

Hata hivyo, hafla ya kuapishwa kwa viongozi hao imefanyika katika Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Makamu wa Rais. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Yustino Ndugai, Katibu Mkuu Kiongozi Balozi John Kijazi, Mawaziri, viongozi wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama na viongozi wa Mkoa wa Dodoma wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa huo Dkt. Binilith Satano Mahenge

 

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Septemba 13, 2018
DC Chongolo azindua zoezi la uandikishaji wa vitambulisho