Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli amewatunuku kamisheni maofisa wanafunzi 146 wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) kuwa na cheo cha Luteni Usu Ikulu jijini Dar es Salaam baada ya kuhitimu mafunzo ya mwaka mmoja.

Maafisa hao wametunukiwa ukamishna baada ya kupata mafunzo katika Chuo cha Mafunzo ya Kijeshi mkoani Arusha yaliyoanza Machi 12 mwaka 2018.

Aidha, waliotunukiwa kamisheni na Rais Magufuli ni maafisa wapya wa JWTZ kundi la 65 kwa mwaka 2019 ambapo jumla yao ni 146, kati yao 140 ni wanaume na sita ni wanawake.

Kwa upande wake mkuu wa chuo cha mafunzo ya Kijeshi mkoani Arusha, Bregadia Jenerali Steven Mkande amesema kuwa kati ya idadi hiyo ya maafisa waliotunukiwa kamisheni watatu wana shahada ya uzamili, 116 wana shahada ya kwanza na mmoja ana stashahada ya uzamili.

Stashahada ya juu ina maafisa watatu huku madaktari wakiwa 23 kati yao 21 ni madaktari wa kawaida wa binadamu na wawili ni madaktari wa wa kinywa na meno.

Hata hivyo, hafla hiyo ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali ikiwemo Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, mawaziri mbalimbali pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda.

Dkt. Mpango aagiza fungu la Lishe lisiguswe
Hatari! Upasuaji chanzo kikuu vifo Wanawake