Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameendelea kung’ara kimataifa katika mapambano dhidi ya rushwa na utawala bora.

Hayo yamesemwa jijini Dodoma na Mkurugenzi Idara ya Habari na Msemaji Mkuu wa Serikali, Dkt. Hassan Abbasi wakati akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu utekelezaji wa masuala mbalimbali ya Serikali.

Amesema kuwa, kimataifa Rais Magufuli amekuwa akiipatia heshima kubwa nchi ya Tanzania kwa mapambano yasiyokoma dhidi ya rushwa hivyo taasisi za kimataifa ikiwemo TRANSPARENCY INTERNATIONAL zimeonyesha Tanzania inaendelea kufanya vizuri katika miaka hii mitatu ikitoka nafasi ya 117 hadi 99.

“Kutokana na utendaji wa kimageuzi wa Rais Magufuli, licha ya juhudi za watu wachache kuhaha kutaka kuichafua nchi yetu kimataifa, Tanzania imeendelea kuwa na taswira nzuri na heshima kubwa na ikiendelea kukubalika sana miongoni mwa Mataifa mbalimbali” amesema Dkt. Abbas

Aidha, Dkt. Abbasi ameongeza kuwa, Novemba, 2018 Serikali ya Nigeria ilitoa Tuzo ya Uongozi Bora kwa viongozi mbalimbali duniani akiwemo Rais Magufuli, mara baada ya Maonyesho ya Kimataifa ya Sanaa na Ufundi yaliyofanyika nchini humo.

Akizunguza kuhusu hali ya uchumi nchini Dkt. Abbasi ameeleza kuwa, Serikali inaamini Mwaka huu 2019 ukuaji wa uchumi nchini utafika asilimia 7.2 na kuifanya Tanzania kuendelea kuwa katika mataifa matano Afrika kwa uchumi unaokua kwa kasi na kuendelea kuwemo katika 10 ya dunia.

Hata hivyo, Dkt. Abbasi amesema kuwa Serikali itaendelea kutekeleza kwa kasi wajibu wake kwa umma ikiwemo kuhakikisha hali ya amani, utulivu, kusimamia utawala bora na utawala wa sheria

Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Februari 6, 2019
Serikali Yatoa notisi ya Siku 24 Kuhuisha Machapisho