Katika kipindi cha miaka Hamsini iliyopita, dunia imeshuhudia ongezeko kubwa la uzalishaji wa bidhaa za plastiki, ambapo katika mwaka 2013, jumla ya tani Milioni 299 Milioni za plastiki zimezalishwa duniani ikiwa ni ongezeka la asilimia 4% ikilinganishwa na uzalishaji wa mwaka 2012.

Kwa mujibu wa Shirika la Uhifadhi Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP) matumizi ya plastiki yameongezeka duniani kutoka tani Milioni 5.5 katika miaka ya 50 hadi tani Milioni 110 Milioni mwaka 2009.

Licha ya kuongezeka kwa uzalishaji wa plastiki kwa kiwango kikubwa, kiwango cha taka za plastiki zinazovurugwa kwa matumizi mengine ni madogo ukilinganisha na uzalishaji, kwani matumizi ya bidhaa za plastiki yamekuwa yakiongozeka kwa kasi na kuchukua nafasi ya bidhaa za chuma na vigae zilizokuwa zikitumika kabla.

Uchafuzi wa mazingira unaotokana na taka za plastiki huathiri na kuharibu mazingira ya miji, ardhini, mito, maziwa, mashambani na hata bahari na pia kutokana na kuenea kwa taka hizo, viumbe kadhaa wa baharini huathiriwa na kemilaki zitokanazo na taka hizo au kwa kula mabaki ya plastiki.

Katika kuunga mkono juhudi za Jumuiya ya Kimataifa za kupinga matumizi ya bidhaa za plastiki ikiwemo mifuko, Serikali ya Tanzania kupitia Ofisi ya Makamu (Muungano na Mazingira), imetangaza kuwa ifikapo Juni mosi mwaka huu, itakuwa ni marufuku kutengeneza, kuingiza, kuuza na kutumia mifuko ya plastiki kwa ajili ya kubebea bidhaa za aina yoyote na matumizi yake yatakoma ifikapo Mei 31, 2019.

Akizungumza na waandishi wa vyombo vya habari Jijini Dodoma, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Balozi Joseph Sokoine anasema Serikali imekuwa ikitoa taarifa mbalimbali ili kuwaelimisha wananchi kuhusu katazo hilo kupitia magazeti, televisheni, redio, mitandao ya kijamii, pamoja wadau na mikusanyiko ya watu ikiwa ni pamoja na taarifa kusomwa katika nyumba za ibada.

Balozi Sokoine amesema kuwa Serikali imeandaa kanuni za utekelezaji wa katazo hilo zitakazoanza kutumika tarehe 1 Juni 2019, ambapo kanuni zitatoa maelekezo mbalimbali kwa ajili ya kupiga marufuku kuzalisha, kuingiza, kusambaza na kutumia mifuko ya plastiki iliyotajwa katika Katazo hilo,  ambapo kiwanda, Kikundi cha Watu au Mtu Binafsi atakayebainika kukiuka matakwa ya Kanuni hizi atakuwa ametenda kosa la jinai na hivyo sheria itachukua mkondo wake.

Ameongeza kuwa Ofisi ya Makamu wa Rais tayari imetoa maelekezo mahsusi kwa Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhusu utekelezaji wa katazo hilo ambapo baadhi yao wameanza kutenga maeneo maalumu kwa ajili ya uhifadhi wa shehena ya mifuko itakayosalimishwa.

“Kwa kushirikiana na Makampuni ya Simu ya Vodacom, Tigo, Airtel na Halotel tumefanikiwa kutuma ujumbe mfupi kwa njia ya simu kwa watumiaji wa mitandao hiyo ambapo watumiaji milioni 11 wa Tigo, Milioni 15.5 wa Vodacom wameshapata ujumbe huu, hii itakuwa endelevu kila wiki,”amesema Balozi Sokoine.

Akifafanua zaidi, Balozi Sokoine amesema Serikali imeendelea kufanya juhudi mbalimbali katika kutoa matangazo kwa kutumia vipaza sauti katika ngazi ya Kata, Mitaa na Vijiji pamoja na kufanya vipindi maalum katika vyombo vya habari ikiwemo kutumia redio za kijamii na redio za mikoani katika kutoa matangazo juu ya katazo hili.

Aidha Balozi Sokoine amesema jitihada zote hizi zinapaswa kuungwa mkono na si kubezwa kwa kuwa ifikapo tarehe 1 Juni 2019, Serikali itaendesha operesheni kabambe nchi nzima ya kusaka mifuko hii na operesheni hiyo itahusisha Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na Wilaya, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali.

Kwa mujibu wa Balozi Sokoine kikosi kazi hicho pia kitaongozwa Shirika la Viwango Nchini (TBS), Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (DPP), pamoja na Mamlaka za Viwanja vya Ndege (TAA), Bandari, Forodha, Uhamiaji, na Usafiri wa Nchi Kavu.

Kuhusu maeneo yatakayotumika kwa ajili ya kusalimisha mifuko ya plastiki, Balozi Sokoine amesema Serikali itatoa utaratibu wa mahali rasmi wanapotakiwa kusalimisha shehena ya mifuko watakayokuwa nayo kwa wale ambao watakuwa tayari kusalimisha kwa hiari.

“Kwa taarifa zaidi kuhusu utekelezaji wa katazo hili Wananchi kwa ujumla mnashauriwa kutembelea Ofisi za Kanda za Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) zilizopo Dar es Salaam, Mtwara, Dodoma, Mbeya, Mwanza, Kigoma na Arusha na pia wanaweza pia kuwasiliana na Wakurugenzi wa Halmashauri za Majiji, Manispaa Miji na Wilaya.

ili kutimiza azma ya kupiga marufuku matumizi ya mifuko ya plastiki ni wajibu wa wadau wote wa mazingira wakiwemo wajasiriamali na wawekezaji na ili kupata maoni kuhusu namna ya kujenga mazingira wezeshi kwa wadau kuwekeza zaidi katika uzalishaji wa mifuko mbadala.

INBAR Yaitaka Tanzania kuweka mkazo kwenye biashara ya Mianzi
Kafulila asitisha mkataba na TBA ujenzi wa nyumba za viongozi Songwe