Wababe wa Jiji la Tanga Coastal Union FC wamejinasibu kuwa tayari kwa mchezo wa Fainali Kombe la Shirikisho Tanzania Bara ‘ASFC’ utakaopigwa Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha, kesho Jumamosi (Julai 02).

Coastal Union ilitinga hatua ya Fainali kwa kuibanjua Azam FC kwa changamoto ya mikwaju wa Penati katika Uwanja huo Mei 29, hivyo kesho itakua na kazi ya kumalizia, dhidi ya Mabingwa wa Tanzania Bara Young Africans.

Kocha Mkuu wa klabu hiyo Juma Mgunda amesema, amekiandaa vizuri kikosi chake, na kipo tayari kupambana na Young Africans (Wananchi), ambayo tayari imeshawasili jijini Arusha tangu jana Alhamis (Juni 30).

“Tuko tayari kucheza na hiyo timu yenu ya Wananchi, tumejiandaa vizuri kwa ajili ya kupambana, tunaamini yaliyopita huenda yakawa yanatumika kama sehemu ya kutushusha kuelekea mchezo wa kesho, ila nikwambieni hatuna wasiwasi na tutapambana kwa mipango wa kushinda.”

“Tumepoteza michezo yote miwili ya Ligi Kuu dhidi ya Young Africans, kwangu ninaamini yaliyopita yameshapita na hatuwezi kuingizwa mkenge kwa kuaminishwa, eti tulipoteza na kesho tutapoteza tena, huu ni mchezo wa Fainali lolote linaweza kutokea, na ndio maana tupo hapa.” Amesema Juma Mgunda

Mchezo wa Fainali umepangwa kuchezeshwa na Mwamuzi Ahmed Arajiga kutoka mkoani Manyara, akisaidiwa na waamuzi Frank Komba (Dar es salaam) na Janeth Balama (Iringa), huku Ramadhana Kayoko akitajwa kama Mwamuzi msaidizi.

Uongozi Simba SC wamkingia kifua Barbara Gonzalez
Nasreddine Nabi: Tutacheza kwa tahadhari kubwa