Ray C anaamini zama zake huenda zilibebwa na vuguvugu la ujana lililomtupa anakokuita ‘jehannam’. Lakini mtikisiko uliowakuta wakali wa zama hizo akiwemo Juma Nature umemfanya akune kichwa bila majibu.

Mwimbaji huyo ambaye sauti yake ya ndege tetere ilikuwa ikisindikizwa na mrindimo wa nyonga zilizoleta utata wa uwepo wa mifupa kiunoni mwake amedai kuwa anahisi kuna ‘jini’ linalowapoteza wasanii wakongwe kwenye ulimwengu wa Bongo Fleva.

Kupitia ujumbe wake alioweka Instagram akiambatanisha na picha ya Lady Jay Dee ambaye tukio la kubadili ukumbi ghafla wa tamasha lake la ‘Naweza’ lilimuamsha akiamini alichezewa mchezo mchafu, Ray C alihoji walikopotelea wasanii kama Mandojo & Domo Kaya, Marlow, Makamua, Matonya, Joselin, Bushoke, Z- Anton na wengine.

“Kuna nini kwenye bongo flava??? wasanii wapya ni wengi yes nalijua hilo lakini ukweli ni kuwa nchi yoyote hapa Africa mashariki nikienda naskia tu nyimbo za zamani nyingi na mpya pia!!mi mwenyewe pamoja na mahanjumat ya pepo ya ahera yote lakini bado sauti ipo na nyie je???Nahisi kuna jini mmoja kwenye hii industry anaesababisha wasanii wengi wajione kama ndo basi tena!point yake ni moja… Nina uwezo wa kukujenga na kukumaliza mara moja!!!maana yake nini sasa???Mungu anisamehe nianze kwenda kabla ya huyu jini!”

Ray C aliwataka wasanii kutokatishwa tamaa na mtu aliyedai kuwa ni promota ambaye anajali zaidi tumbo lake ambaye hata hivyo hakumtaja jina.

“Wasanii mna kazi kubwa ya kuanza kujiamini kwanza kabla ya kuamini mtu mwingine!Mkishajua aliewapa vipaji naamini Mtasimama tena,Mtaingia studio tena!Maana mashabiki wenu bado wapo!!!Kinachohitajika ni kipaji sio promota anaefikiria tumbo lake na mpaka leo anazidi kukondeana!! Ziba lakini tutakutana kaburini!” alimaliza.

‘Unanimaliza’ ulikuwa wimbo mkubwa wa Ray C uliotoka mwaka 2017 na kuwakumbusha wapenzi wa Bongo Fleva kuwa malkia wa sauti na viuno anaweza kurudia taji lake.

Tottenham kumzawadia Ponchettino Mkataba mnono.
Afrika kusini yaomboleza kifo cha Winnie Mandela.