Kocha wa Liverpool, Jurgen Klopp ameonya kuwa wachezaji wa AS Roma hawatakuwa na subira wala kumchekea mchezaji mwenzao wa zamani, Mohamed Salah katika mechi ya mzunguko wa nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Barani Ulaya, utakaoziumiza nyasi za Anfield, leo.

Alipokuwa Roma, Salah alifanya vyema kwa kuifungia timu hiyo magoli 34 katika mechi 83 alizoshiriki kabla ya kuhamia Liverpool alipong’ara zaidi.

Leo itakuwa mara ya kwanza kwa Salah kucheza dhidi ya timu yake hiyo ya zamani, akivutana na kuminyana na waliokuwa wachezaji wenzake.

“Nadhani Mo atafahamu hivi punde kuwa wale sio wachezaji wa timu yake tena,” alisema Klopp.

“Safu za ulinzi za wachezaji wa Italia ni maarufu kwa kutoonesha mchezo wa kirafiki. Lakini anaweza kupambana kwa misingi ya mpira wa miguu,” aliongeza.

Salah ameifungia Liverpool magoli 41 kati ya mechi 46 alizoshiriki. Jumapili iliyopita alitangazwa kuwa mshindi wa tuzo ya Mwanasoka bora wa England kwa msimu wa 2017/18.

Alikabidhiwa tuzo hiyo, maarufu kama ‘PFA-Player of the Year’, kutokana na jinsi alivyoonesha kiwango cha juu akipachika jumla ya magoli 31 kwenye ligi.

Klabu ya Liverpool, leo wanakibarua cha kujaribu kuingia katika fainali za Ligi ya Mabingwa kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2007.

UK yatoa tahadhari juu ya maandamano ya April 26
Zoezi la usambazaji gesi majumbani kuanza rasmi leo