Mabingwa wa soka nchini Italia klabu ya Juventus, wamethibitisha kumsajili moja kwa moja mshambuliaji wa pembeni kutoka Brazil Douglas Costa.

Juventus wamekamilisha dili ya mshambuliaji huyo, baada ya kumtumia kwa mkopo msimu uliopita akitokea kwa mabingwa wa soka nchini Ujerumani FC Bayern Munich.

Pande hizo mbili zimefikia makubaliano ya usajili wa mshambuliaji huyo, ambao umewagharimu Juventus Euro milioni 40 sawa na Pauni milioni 35.2.

Costa mwenye umri wa miaka 27, amesaini mkataba wa miaka minne ambao utamuwezesha kuitumikia Juventus hadi mwaka 2022.

Msimu uliopita Costa aliifungia mabao sita na kutoa pasi 14 za mwisho katika kikosi cha Massimiliano Allegri, huku akichangia kwa kiasi kikubwa mafanikio ya kutetea taji la ligi na kutwaa ubingwa wa 13 wa kombe la Italia (Coppa Italia).

Costa kwa sasa yupo kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Brazil, kinachojiandaa na fainali za kombe la dunia, zitakazoanza rasmi Juni 14 nchini Urusi.

Liverpool walazimisha usajili wa Nabil Fekir
Urusi 2018: Nani atabeba Kombe? Tuimulike Korea Kusini