Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, imefanya ukaguzi wa miradi mitatu ya uboreshaji wa miundombinu ya kitalii ya ujenzi ya Barabara ya kilometa 47.5, lango kuu la kuingilia wageni na eneo la kupumzikia watalii wenye gharama ya Shilingi Milioni 672.

Akizungumza baada ya ukaguzi wa miradi hiyo iliyopo katika pori la akiba la Mkungunero la Mikoa ya Dodoma na Manyara, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya bajeti, Daniel Sillo amemshukuru Rais, Samia Suluhu Hassa kwa kufanikisha upatikanaji wa fedha hizo.

“Lakini pia nipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), kwa usimamizi mzuri wa miradi na pia nasisitiza muendelee kusimamia matumizi ya fedha za miradi ya maendeleo,” amesema Sillo.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, iikipewa maelezo wakati wa ukaguzi wa miradi mitatu ya uboreshaji wa miundombinu ya kitalii katika pori la akiba la Mkungunero lililopo Mikoa ya Dodoma na Manyara

Awali, akiongea katika eneo hilo Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja amesema uboreshwaji wa miundombinu katika Pori la akiba Mkungunero, utatoa wigo mpana wa eneo hilo kutembelewa na watalii.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na utalii, Prof. Eliamani Sedoyeka ameipongeza TAWA kwa kufanikisha zoezi la uboreshwaji huo wa miundombinu na kuishukuru Kamati ya kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa kutenga muda kwa ajili ya kupitia miradi hiyo.

Kwa upande wake, Kaimu Naibu Kamishna wa Uhifadhi, Mlage Kabange amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha hizo kwa muda muafaka, wakati Taifa likijiandaa kupokea wageni wengi baada ya uzinduzi wa filamu maalumu ya “Royal Tour”.

Askari wa kada mbalimbali wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya bajeti, Daniel Sillo wakati alipotembelea pori la akiba la Mkungunero la Mikoa ya Dodoma na Manyara.

Miradi hiyo, imejengwa kupitia fedha za Mradi wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19.

Maliasili na Utalii 'watisha' matumizi ya fedha za umma
Habari kuu kwenye magazeti ya leo Julai 06, 2022