Uchambuzi wa taarifa ya mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali unatarajia kufanyika hivi karibuni kufuatia Vikao vya Kamati 14 za Kudumu za Bunge kuanza Jumatatu Oktoba 21, 2019 na kuendelea hadi Novemba 1, 2019 Jijini Dodoma.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na kitengo cha mawasiliano na uhusiano wa kimataifa ofisi ya Bunge Dodoma imesema uchambuzi wa taarifa hiyo utahusu hesabu zilizokaguliwa za Serikali za mitaa na Serikali Kuu kwa mwaka wa Fedha unaoishia Juni, 2018.

“Shughuli zote za Kamati katika kipindi hicho zimepangwa kwa kuzingatia kanuni za kudumu za Bunge toleo la Januari 2016 na zitahusisha kupokea na kujadili taarifa ya mapendekezo ya mwongozo wa kutayarisha mpango wa maendeleo wa Taifa na bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2020/2021,” imesema taarifa hiyo.

Imesema shughuli nyingine ni pamoja na uchambuzi wa taarifa ya msajili wa hazina kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma katika mashirika na taasisi mbalimbali nchini na uchambuzi wa taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Wizara na taasisi mbalimbali za Serikali.

Aidha taarifa hiyo ya Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano wa Kimataifa Ofisi ya Bunge pia imesema uchambuzi wa Sheria ndogo zilizowasilishwa wakati wa mkutano wa 16 wa Bunge pia utafanyika.

TMA yatangaza mvua kubwa siku mbili
Hizi hapa nafasi za kazi kutoka makampuni 10 Tanzania