Shirika la Koyo la kutoka Japan limepania kuwekeza kwenye miundombinu ya umeme wa gesi asilia na umeme jua ili kuleta maendeleo ya haraka kwa wananchi waishio vijijini.

Hayo yamesemwa jana jioni (Jumatatu, Mei 9, 2016) na Mwenyekiti na Mtendaji Mkuu wa shirika la Koyo, Bw. Norio Shoji wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ofisini kwake, Magogoni, jijini Dar es Salaam.

“Tumepanga kuwekeza kwenye maeneo matano ambayo mojawapo ni kujenga mtambo wa kuchakata gesi kwa kutumia gesi asilia inayozalishwa hapa nchini. Mtambo huu utakuwa na uwezo wa kuzalisha megawati 1,000 za umeme,” alisema.

“Pia tunao mpango wa kujenga mitambo ya umemejua inayoweza kujiunganisha kwenye gridi (on-grid/off grid solar power plants) kwa ajili ya maeneo vijijini  na yale yasiyofikika kwa urahisi zaidi ikiwa ni pamoja na kuboresha mfumo wa usambazaji umeme kwenye gridi ya Taifa ili Tanzania iweze kuzalisha zaidi nishati hiyo na kuiuza nchi jirani,” aliongeza.

Bw. Shoji alimweleza Waziri Mkuu kwamba wana nia ya kuwekeza pia katika sekta nyingine kama kilimo, sayansi ya tiba (medical science), usafishaji na uyeyushaji madini (refinery-smelting), uzalishaji wa bidhaa za viwandani na teknohama.

Akifafanua zaidi Bw. Shoji alisema shirika lake kwa kushirikiana na makampuni mengine makubwa ya Japan pamoja na Serikali ya nchi hiyo wamedhamiria kuwekeza kwenye miundombinu hiyo kwa sababu wanataka Tanzania iwe ni kitovu (hub) cha uzalishaji na iweze kulisha nchi jirani katika SADC na EAC.

Akitolea mfano, Bw. Shoji alisema mbali na miradi mingine wanayotaka kuwekeza, gharama za kuweka mtambo wa kuzalisha megawati 1,000 za umeme hazitapungua kiasi cha dola za marekani bilioni moja (sawa na sh. trilioni 2.2).

Waziri Mkuu alimshukuru Bw. Shoji kwa nia yake aliyoionyesha na akamtaka achangue eneo mahsusi kwa sababu Tanzania inahitaji umeme wa kutosha katika kutekeleza azma yake ya kuwa nchi ya uchumi wa viwanda.

“Serikali ya awamu ya tano imedhamiria kujenga uchumi wa viwanda ili kuongeza ajira na kuondoa umaskini miongoni mwa wananchi wake. Tunahitaji uwekezaji mkubwa kwenye nishati ya umeme katika mikoa ya Kusini, ya Kaskazini, ya Magharibi na hata mikoa ya kati,” alisema Waziri Mkuu.

Kwa upande wake, Bw. Suleiman M. Nassor alisema shirika la Koyo litafanya uwekezaji huo kwa kushirikiana na kampuni ya SSF Limited ambayo inajihusisha na masuala ya nishati.

“Tunashirikiana na shirika la Koyo pamoja na Serikali ya Japan ili kuleta unafuu wa maisha kwa Watanzania wenzetu,” alisema Bw. Nassor.

Theo Walcott Achoshwa Mfumo Wa Babu Arsene Wenger
Danny Welbeck Kuzikosa Fainali Za Ulaya (Euro 2016)