Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi CUF, Khalifa Suleiman Khalifa amesema kuwa chama hicho hakiwezi kufa kwasasa kutokana na uongozi mpya ambao umeingia madarakani kuwa unaongozwa na Mwenyekiti wake Profesa Ibrahim Lipumba.

Ameyasema hayo jijini Dar es salaam wakati akizungumza na kituo kimoja cha redio kuhusu wafuasi wa chama hicho kuhamia ACT- Wazalendo, ambapo amesema kuwa CUF haiteteleki kwakuwa wale walioondoka ni wasaliti.

“CUF haielekei shimoni, bali inaelekea kwenye mafanikio kwa sababu wale wasaliti washaondoka ndani ya chama chetu, kuhusu kushinda Wabunge wengi kwasasa bado ni mbali sana maana unaweza kuungwa mkono na watu wengi lakini kwenye sanduku la kura ukashindwa,” amesema Khalifa.

Amesema kuwa hajui watu wanaposema kuwa kuvaa viatu vya Maalim Seif wanazungumzia kitu gani, kama ni kufanya majukumu ambayo alikuwa anafanya, atahakikisha anajenga ushawishi mkubwa kushinda wa Maalim Seif.

Hata hivyo, siku za hivi karibuni, Khalifa alisema katika kuhakikisha CUF mpya inazaliwa ina mpango wa wakushirikiana na baadhi ya viongozi wenzake wa vyama vya upinzani pamoja na Chama Cha Mapinduzi CCM.

 

Video: Polisi wala sahani moja na ACT Dar, Mahakama ya Mafisadi yaanza kazi kwa kishindo
Hongereni kwa kufikia hatua hii ya Ujenzi- Majaliwa