Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola ametoa maelekezo kwa Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua za kisheria madereva wa magari ya viongozi watakaovunja sheria za usalama barabarani kama ilivyo kwa wengine.

Ameyasema hayo jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari, saa chache baada ya Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla kupata ajali iliyomsababishia majeraha na kuchukua uhai wa ofisa habari wa wizara hiyo, Hamza Temba (32).

Wengine waliojeruhiwa katika ajali hiyo iliyotokea jana alfajiri, ni wasaidizi wa waziri huyo, Michael Lingwa (30) na Ramadhani  Magimba (30).

Aidha, ajali hiyo ilitokea wakati dereva akimkwepa twiga aliyeingia ghafla barabarani katika barabara kuu ya Arusha – Dodoma, Kijiji cha Mdori wilayani Babati.

Hii ni ajali ya pili kutokea ndani ya wiki hii, zote zikihusisha magari ya Serikali na kusababisha vifo, majeruhi na kupoteza fedha za walipakodi zilizotumika kuyanunua.

“Madereva wa magari ya Serikali wanaongoza kwa kutanua barabarani na mwendokasi, Jeshi la Polisi liwachukulie hatua za kisheria madereva hao kama watu wengine,” amesema Lugola.

Hata hivyo, kauli ya waziri huyo, iliungwa mkono na Mjumbe wa Baraza la Usalama Barabarani, Hamza Kasongo ambaye amesema kuwa dereva akiwa anaendesha STK au STL huwa anajiona ‘special’ (maalumu) sana na kuvunja sheria za barabarani.

 

Majaliwa akunwa na Makumbusho ya Taifa
Mhagama awafunda watumishi ofisi ya mpiga chapa wa Serikali