Waziri wa Mambo ya Ndani, Kangi Lugola amekutana na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Kimataifa la Kuwahudumia Wakimbizi (UNHCR), Chansa Kapaya, jijini Dar es salaam na kujadiliana masuala mbalimbali ya wakimbizi nchini.

Lugola pamoja na Mwakilishi huyo, pia walijadiliana masuala ya ushirikiano kati ya Serikali na Shirika hilo la Kimataifa kwa mujibu wa sheria zinazowaongoza.

Amesema kuwa wizara yake haiwezi ikafanikiwa kikamilifu katika masuala ya kuwahudumia wakimbizi nchini kama haitashirikiana ipasavyo na UNHCR.

“Licha ya kuwa baadhi ya wakimbizi wanaendelea kurudishwa kwa hiari nchini kwao Burundi, lakini katika kufanikisha zoezi hili, lazima tushirikiane ipasavyo kati ya Serikali pamoja na nyie UNHCR, naamini Wizara yangu itafanya vikao nanyi mara kwa mara ili kufanikisha zoezi hilo pamoja na mengineyo yanafanikiwa,” amesema Lugola.

Kwa upande wake Mwakilishi wa UNHCR, Kapaya, amesema kuwa Serikali ya Tanzania inashirikiana na Shirika lake vizuri, na jambo lolote la majadiliano linapotokea hujadiliana ili kuweka sawa ushirikiano huo.

Katika kikao hicho Mwakilishi wa UNHCR aliambatana na Msaidizi wake Zephania Amuiri, na Waziri Lugola aliambatana na Mkurugenzi wa Idara ya Wakimbizi wa Wizara yake, Harrison Mseke.

Video: Zitto amvimbia Spika kuhusu CAG, sasa kumburuza Mahakamani
Kwandikwa ahimiza ushirikiano kutatua changamoto za elimu