Rapa Kanye West ameamua kufanya ambacho wengi hawakutarajia wakati wakiendelea kusubiri kwa hamu albam yake ijayo iliyotanguliwa na matukio mengi yaliyolifanya jina lake kuwa gumzo mitandaoni, kwa kutangaza kuweka kwenye albam hiyo picha ya daktari aliyemfanyia mama yake upasuaji siku moja kabla ya kifo chake.

Mbabe huyo wa mistari na tungo tata ameweka wazi uamuzi huo alipokuwa anamjibu mmoja kati ya mashabiki wake kwenye jumbe walizokuwa wakitumiana.

Dkt. Jan Adams alimfanyia upasuaji mama Kanye West mwaka 2007 siku moja kabla ya kifo chake, lakini Kanye aliweka chuki dhidi yake akiamini ni sehemu ya chanzo.

“Hii ndiyo ‘cover’ ya albam yangu, huyo ni Dkt. Jan Adams. Mtu aliyemfanyia mama yangu upasuaji wa mwisho,” aliandika Kanye West, ingawa hakutaja moja kwa moja jina la albam hiyo.

Kanye anadai kuwa ameamua kusamehe na anataka kuwapa changamoto na wengine ambao wana watu wanaowachukia kuweka kando chuki zao na kuwasamehe.

“Leo niina changamoto kwa kila mmoja wenu. Chagua mtu mmoja ambaye ulikuwa na tofauti naye, ambaye unadhani unamchukia na hata mtu ambaye hata ulikuwa hauongei naye kwa miaka. Wasiliana na mtu huyo na mwambe ‘nakupenda’,” aliandika.

Albam mpya ya Kanye West inatarajiwa kuingia sokoni Juni 1 mwaka huu. Ijumaa wiki hii, Kanye aliachia nyimbo kadhaa ikiwa ni pamoja na Lift Yourself na Ye vs. the People aliyomshirikisha T.I.

Mama Salma amwaga nasaha nzito kwa Ali Kiba na Abdu 'Simu ni mtihani'
Aliyeanzisha kampeni ya kumng'oa Rais avurugwa