Katibu Mkuu wa Simba, Anord Kashembe amewataka Mashabiki na Wanachama wa klabu hiyo kutulia katika kipindi hiki na kuuwaacha viongozi wafanye kazi yao ya kuboresha kikosi kwa ajili ya msimu mpya wa Ligi Kuu pamoja na Ligi ya Mabingwa Afrika.

Kashembe ametoa kauli hiyo baada ya klabu ya Simba kuwatambulisha baadhi ya wachezaji kuanzia mwishoni mwa juma lililopita hadi jana jioni, ambapo walimtambulisha mshambuliaji wa kutoka DR Congo Chris Mugalu akitokea Lusaka Dynamos ya Zambia.

Amesema kazi iliyo mbele ya viongozi wa Simba SC kwa sasa, ni kuhakikisha wanafuata mapendekezo na maelekezo yaliyowasilishwa mbele yao kupitia ripoti ya benchi la ufundi, linaloongozwa na kocha Sven Vandenbroeck, ambaye tayari amesharejea nchini akitokea nyumbani kwao Ubelgiji, baada ya kumaliza likizo ya mapumziko mafupi.

“Mashabiki na wanachama wanatakiwa kutulia, viongozi wanafanya usajili wa wachezaji kulingana na mapendekezo ya kocha pia mahitaji ya timu yetu, kwa msimu huu tunataka kucheza fainali ya Ligi ya Mabigwa,” amesema Kashembe.

Amesema kikosi chao kinatarajia kuanzia mazoezi leo Jumatatu katika Uwanja wa Mo Simba Arena chini ya Kocha Mkuu Sven Vandenbroeck sambamba na wasaidizi wake.

Kashembe amesema wameona makosa yao ya msimu uliopita katika michuano ya kimataifa na Ligi Kuu, na ndio maana wamesajili kulingana na ripoti ya benchi la ufundi ilivyoelekeza.

Amesema mbali na usajili huo pia malengo makubwa ni kufanya maboresho madogo katika kikosi pamoja na kumwongezea mkataba kocha Sven Vandenbroeck.

“Baadhi ya wachezaji wetu waliokwenda likizo wanatarajia kurejea ndani ya siku hizi mbili, kuingia kambini kwa ajili ya maandalizi ya mechi yetu ya Ngao ya Jamii na msimu mpya wa ligi unaotarajia kuanza hivi karibuni, Sven ataendelea kuwa kocha wetu, hatuwezi kumuacha,” amesema.

Mbali na mshambuliaji Mugalu, wengine waliothibitishwa na klabu hiyo katika kipindi hiki ni pamoja winga Mghana Bernard Morrison (mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba na Yanga), beki wa kati Mkenya Joash Onyango ambaye ni mchezaji huru baada ya kumaliza mkataba wake wa Gor Mahia ya kwao Kenya na straika Mzambia Larry Bwalya kutoka Lusaka Dynamos.

Kwa upande wa wachezaji wa ndani ni beki wa kati Ibrahim Ame aliyetokea Coastal Union ya Tanga, David Kameta ‘Duchu’ (Lipuli FC)na Charles Ilamfya kutoka KMC FC.

Viongozi wa dini wakemea vurugu, matusi Uchaguzi Mkuu
SADC kuimarisha mfuko wa dharula kupambana na majanga