Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimemtaka Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia kumuomba radhi Mbunge na Mwanasheria Mkuu wa Chama hicho, Tundu Lissu bila hivyo wametangaza moja ya mambo watakayofanya ni kuhamasisha wanachama wake kutoshiriki shughuli za TFF.

Chadema wametoa tamko hilo ikiwa ni saa chache baada ya Rais wa TFF kulitaja jina la Mbunge huyo wa Singida Mashariki katika mkutano wa mwaka wa Shirikisho hilo uliofanyika jijini Arusha.

Aidha, katika taarifa yao CHADEMA wameandika kuwa wamepokea kauli yenye ukakasi mkubwa iliyotolewa na Rais wa Chama cha Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia kuwa atawashughulikia wale wote ambao wataleta ” U-Tundu Lissu” kwenye mpira.

“Sasa kauli ya Karia inatufanya tujiulize maswali mengi kama vile, inawezekana anawajua waliomshughulikia Tundu Lissu na ndio maana anataka kuwatumia kushughulikia ‘Tundu Lissu’ walioko kwenye mpira,”imesema taarifa hiyo

Taarifa hiyo imesema kuwa Chadema wako tayari kusimamisha mahusiano na ushirikiano wowote na TFF ikiwemo kuwataka Wanachama wao kutokushiriki matukio yote yanayoandaliwa na TFF, kususia bidhaa zote zenye nembo au zinazotolewa na TFF zikiwemo jezi za timu za Taifa na nyinginezo.

Hata hivyo, taarifa hiyo imeongeza kuwa itachukua hatua kali dhidi ya makampuni ambayo yataendelea kushirikiana na TFF ikiwemo kususia bidhaa zao, kwani watakuwa wanaunga mkono taasisi inayoongozwa kwa ubaguzi wa kisiasa, kuwashawishi wadau wa mpira kokote kusitisha mahusiano na TFF, hivyo wamemtaka Karia kuomba radhi.

Mahakama ya ICC yamuombea hifadhi Gbagbo Ubelgiji
Habari kubwa katika magazeti ya Tanzania leo Februari 3, 2019