Serikali imesema imejipanga kuhakikisha inatekeleza mpango wa kunusuru kaya masikini katika awamu ijayo kwa kuzifikia kaya milioni 1.4 ili kutokomeza umasikini nchini.

Akiongea na waandishi wa habari, Waziri wa nchi ofisi ya Rais menejimenti ya utumishi wa umma na utawala bora, John Mkuchika amesema mwaka huu wamelenga kuzifikia halmashauri 185 zilizopo Tanzania bara na visiwani.

Amesema tangu mpango huo uanzishwe mwaka 2012, hadi sasa jumla ya kaya milioni 1.1 bara na visiwani zimefikiwa na mpango huo lakini kuna baadhi ya maeneo bado hayajafikiwa.

“Takwimu zinaonyesha umasikini wa mahitaji ya msingi kwa kaya za walengwa umepungua kwa asilimia 10 na ule uliokithiri kwa asilimia 12 kwa kaya masikini sana” amesema Mkuchika.

Ameongeza kuwa utekelezaji wa mpango huo umewezesha kaya za walengwa kujikita kwenye shughuli za kukuza kipato na kujiimarisha kiuchumi ikiwamo ufugaji, uvuvi, kilimo na biashara ndogondogo.

Mkurugenzi mtendaji wa Tasaf, Ladislaus Mwamanga amesema ili kuepukana na udanganyifu kwa awamu hii wameboresha mifumo na kuiweka iwe ya kidigitali na tayari wameifanyia majaribio wilaya tatu za Mtwara, Nanyumbu na Siha na mfumo umefanya vizuri.

Aidha katika awamu hiyo mpya jumla ya Sh. Trilioni mbili zimepangwa kutumika katika shughuli za kunusuru kaya masikini ambapo hapo awali awamu ya kwanza zilitumika Sh, trilioni 1.7.

Serikali yamsaka Nabii aliyetangaza kutibu virusi vya Corona
Bwawa la nyumba ya Mungu hatarini kupasuka