Mahakama ya juu nchini Kenya, imekubali ombi la kupinga matokeo ya Urais yaliyotangazwa na Tume huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini Kenya (IEBC), lililowasilishwa na Kiongozi wa Azimio la Umoja, Raila Odinga kuhusu ushindi wa William Ruto.

Odinga na mgombea mwenza wake Martha Karua, wanatafuta afueni 23 ikiwemo agizo la kukaguliwa kwa seva za IEBC na kuchunguzwa kwa kura zilizokataliwa na kuharibika.

Walalamikaji hao, pia wanataka agizo la uchunguzi na ukaguzi wa kitaalamu wa vifaa vya Kenya vya ‘Integrated Elections Management System (Kiems)’, tovuti ya IEBC na fomu za uchaguzi wa urais zikiwemo Fomu 34A, 34B na 34C.

Aidha, wanataka agizo la kubatilishwa kwa uchaguzi wa Ruto na IEBC kushurutishwa kuandaa uchaguzi mpya wa urais kwa kufuata kikamilifu Katiba na Sheria ya Uchaguzi na kwamba uchaguzi huo mpya utakaoandaliwa usiongozwe na Chebukati.

Wawili hao, pia wanaomba agizo la kumwita Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai, George Kinoti ili kuwasilisha taarifa, picha, ripoti, vifaa, kompyuta mpakato, simu na vifaa vingine vyote vinavyohusiana na uendeshaji wa uchaguzi vilivyokutwa kwa raia wa Venezuela aliyekamatwa Jomo Kenyatta Iinternational Airport (JKIA).

Odinga na Karua, pia wanataka Kinoti aitwe na kuelekezwa kutoa kompyuta ndogo zinazodaiwa kuchukuliwa na kunyakuliwa kutoka kwa Koech Geofrey Kipngosos, wakala wa chama cha UDA na kuripoti uchunguzi wa kompyuta hiyo au hizo na mambo yaliyomo.

Wahanga wa Ugaidi kupewa kipaumbele huduma za jamii
Wananchi 'wajiweka rehani' ajali ya Lori la mafuta