Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kesho Jumatano Julai 25, 2018 anatarajiwa kushiriki zoezi la usafi eneo la Coco Beach pamoja na wananchi na watendaji mbalimbali.

Zoezi hilo ni utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli alilolitoa Juni 29 mwaka huu kwamba Watanzania wafanye usafi kwenye maeneo yao ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa ambayo huadhimishwa Julai 25 kila mwaka.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, wananchi wanatakiwa wafike eneo hilo kuanzia saa 12:30 asubuhi ili waanze shughuli hiyo na usafi huo utafanyika kuanzia kwenye eneo la wafanyabiashara wa mihogo kuelekea maeneo ya Police Officers’ Mess.

Juni 29 mwaka huu, wakati akitoa maelekezo kwenye hafla ya uzinduzi wa kituo cha polisi kinachohamishika, Waziri Mkuu alisema:

“Rais Dkt Magufuli anawataka Watanzania wote waadhimishe siku hiyo ya kumbukumbu ya mashujaa kwa kufanya usafi katika maeneo yaliyo jirani na makazi yao pamoja na yale ambayo wamezikwa mashujaa ikiwa ni njia ya kuwaenzi.

Siku hiyo hiyo, Waziri Mkuu alitangaza kwamba Rais Magufuli ameagiza kwamba sh. milioni 308 zilizotengwa kwa ajili ya maadhimisho ya Siku ya Kumbukumbu ya Mashujaa, zitumike kuboresha miundombinu ya barabara jijini Dodoma.

Aliitaja miundombinu hiyo ni pamoja na taa za kuongozea magari katika barabara ya kisasa na taa za barabarani kwenye barabara mpya ya kutoka Emmaus hadi African Dream yenye urefu wa kilomita 1.4, ambayo kwa sasa inajengwa kwa kiwango cha lami.

Sasa leseni za madereva kuhakikiwa kielektroniki
Madereva wasio na vyeti kufungiwa leseni