Mahakama ya Katiba nchini Uganda imeanza kusikiliza shauri lililowasilishwa mahakamani hapo kupinga jaribio la kubadili katiba na kuondoa ukomo wa umri wa urais.

Mwaka jana, Bunge lilipiga kura ambapo wengi waliunga mkono kuondolewa kwa ukomo wa umri wa kuwa raisi wa nchi hiyo ambao Katiba inaonesha ni miaka 75.

Kwa mujibu wa katiba ilivyo sasa, Rais Yoweri Museveni mwenye umri wa miaka 73 atakosa sifa za kugombea urais mwaka 2021.

Wanasheria wa kambi ya upinzani wamedai kuwa mabadiliko hayo yamevunja sheria na kwamba bunge halikufuata utaratibu walipokuwa wakipitisha muswada huo.

Kesi hiyo inayosikilizwa wiki hii, ulinzi mkali umeshuhudiwa katika eneo la mashariki mwa mji wa Mbale na baadhi ya barabara zimefungwa kuhakikisha hakuna vurugu ya aina yoyote.

Hii ni mara ya kwanza kwa mahakama kusikiliza kesi ya kikatiba iliyovuta umakini wa watu wengi. Awali, ilidaiwa kuwa kesi hiyo ingehamishwa kutoka Kampala kwa lengo la kuepuka umati mkubwa kwenye viunga vya mahakama na mitaani.

Wawasilisha maombi ni wabunge wa upinzani, Chama cha Wanasheria wa Uganda na asasi za kiraia.

Spika ajiuzulu kukwepa kura ya kung'olewa
Marekani kuchukua maamuzi magumu dhidi ya Syria