Mwanasiasa wa upinzani Kenya aliyeidhinisha kiapo cha kiongozi wa upinzani Raila Odinga kuwa Rais wa Wananchi, Januari Miguna Miguna ametimuliwa tena nchini Kenya, huku mzozo kuhusu kesi ya uraia wake ukiendelea.

Miguna ametumia ukurasa wake wa Facebook ameandika kuwa ameamka na kujikuta yuko Dubai na kwamba anahitaji matibabu.

Amesema anafahamu kwamba kuna mpango wa kumpeleka London lakini anataka kupanda ndege ya kurejea Nairobi pekee, Mwanasiasa huyo amesema amesindikizwa na afisa wa idara ya ujasusi.

Serikali imechukua hatua hiyo licha ya kuwepo kwa maagizo ya mahakama ya kuzuia kutimuliwa kwake na kuitaka serikali kufanikisha kurejea kwake nchini humo.

Mawakili wa Miguna wamethibitisha kwamba aliondolewa nchini humo kwa kutumia ndege ya shirika la Emirates iliyokuwa inaelekea Dubai.

Bw Miguna alikuwa amezuiliwa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) tangu alipowasili Jumatatu adhuhuri.

Picha: Miguna alazwa hospitalini
TRA yazindua vitambulisho kwa wafanyabiashara wadogo