Rapa Kghaligraph Jones kutoka Kenya, ambaye anatajwa kuwa moja kati ya marapa ‘hatari’ zaidi Afrika kwa sasa, ameeleza jinsi alivyoingia kwenye bifu na mkali mwenzake Octopizzo.

Akifunguka kwenye XXL ya Clouds FM hivi karibuni, mkali huyo wa ‘Mazishi’ alisema Octopizzo aliwahi kukutana naye kwenye mashindano ya michano mitaani kabla hawajajulikana. Katika shindano mojawapo kubwa, Khaligraph aliibuka mshindi wa michano huru na kumuacha Octopizzo.

Hata hivyo, waliporudi kwenye maisha ya muziki wa mkondo mkuu, Octopizzo alikuwa wa kwanza kung’ara na kupata umaarufu mkubwa. Hivyo, baada ya kuanza kumsikia Khaligraph anapanda ngazi alipata hofu ya biashara yake kwakuwa alijua uwezo wake.

“Ni kama alikuwa intimidated, aliona kama biashara yake sasa inaingiliwa,” alisema Khaligraph ambaye alimpa kampani Young Killer kwenye tamasha jijini Dar es Salaam.

Khaligraph anadai kuwa kutokana na umri wa wakati huo hakuwa anakopesha uvumilivu, alimlipua Octopizzo na mbio za vijiti ikaanzia hapo. Lakini anadai kwa umri alioufikia sasa mambo sio kama yalivyokuwa awali na ndio sababu bifu kati yao imepoa.

Aidha, rapa huyo amedai kuwa katika maisha ya muziki wa hip hop na rap kwa ujumla, ushindani wa uhasama wa ‘nani mkali’ ndio utamaduni wake na huchangamsha mchezo huo, tofauti na watu wengine wanavyodhani.

Khaligraph ameshirikishwa na Young Killer kwenye wimbo ‘Shots’ ambayo tayari imewekwa kwenye video kali. Ngoma hiyo ni ya pili baada ya ‘How We Do’ waliyofanya pamoja.

Mchezo kati ya Simba na Lipuli wapigwa kalenda
Diamond akamatwa, ahojiwa kwa video za faragha