Mahakama ya Hakimu mkazi ya Wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma imemhukumu kifungo cha maisha, mkazi wa kijiji cha chongola, Jevi Msusu(43) baada ya kupatikana na hatia ya kumfanyia ukatili mke wake kwa kumkata kidole cha mkono na kukiondoa kabisa.

Hakimu mkazi wa mahakama ya wilaya Mpwapwa, Paschal Mayumba alisema mahakama imejiridhisha kuwa mtuhumiwa huyo bila uhalali alimjeruhi, Pendo Charles ambaye ni mke wake kwa kumkata kidole chake na kukiondoa.

Msusu alitenda kosa hilo kinyume na kifungu cha sheria namba 222 kifungu kidogo (a) na (b) ya kanuni ya adhabu iliyofanyiwa marejeo mwaka 2002, akisomewa hoja za awali na mwendesha mashtaka wa polisi, Willison Mwita, alidai mtuhumiwa alikiri hoja zote na mahakama haikuwa na hoja za kupiganiwa.

Aidha, mtuhumiwa huyo alipoulizwa kuhusu tuhuma zinazo mkabili alikiri kutenda kosa hilo kwa madai kuwa alipitiwa na shetani, na alipopewa nafasi ya kujitetea alitaka mahakama imsamehe kwa kuwa ana majukumu na familia na watoto wanamtegemea.

Hata hivyo, mwendesha mashtaka wa polisi, Mwita aliomba mahakama itoe adhabu kwa mtuhumiwa kutokana na vitendo vya kikatili vinayoendelea kwa wanawake, na hakimu Mayumba aliiambia mahakama kuwa mtuhumiwa atatumikia kifungo cha maisha jela kutokana na mtuhumiwa mwenyewe kukiri kosa

Arsene Wenger anukia AC Milan
Spika Ndugai aapisha wabunge wanne wa CCM