Vita ya maneno imezidi kukolea kati msemaji wa Timu ya Mtibwa Sugar, Thobias Kifaru na msemaji wa Ruvu Shooting, Masau Bwire, kuelekea mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara utakaozikutanisha timu hizo.

Mtibwa wanatarajia kuwa wenyeji wa Ruvu Shooting Jumatatu ijayo ya Februari 19 katika dimba la Manungu Turiani mkoani Morogoro ambapo kuelekea mchezo huo, Masau Bwire amekuwa akitamba kuendeleza wimbi la ushindi kwa upande wa Ruvu Shooting.

Bwire ambaye timu yake imetoka kushinda mechi tatu mfululizo katika dimba la Mabatini licha ya kupoteza mchezo dhidi ya Simba, amesema hivi sasa timu hiyo imekuja na mtindo mpya wa “Kupapasa”, na kuahidi kwenda “kuipapasa” Mtibwa Sugar nyumbani kwao.

Kufuatia tambo hizo, Thobias Kifaru naye ameibuka na kujibu mashambulizi akiahidi kumtia adabu Masau Bwire kwa kuipa kichapo Ruvu Shooting, akidai kuwa Mtibwa ina uwezo mkubwa kuliko Ruvu Shooting na ina hasira ya kutofanya vizuri katika michezo yake mitatu ya Kanda ya Ziwa.

Kifauru amemtaka Masau kuwa na akiba ya maneno kwani bado ni kijana mdogo na mchanga katika fani hiyo.

“Hao ni vijana wadogo ambao bado wanaigaiga, mimi nipo kwenye hii kazi kwa zaidi ya miaka 30, na sasa nakaribia kustaafu, kwahiyo huyo kijana wangu Masau Bwire atulie, apunguze maneno, lazima nitamfundisha adabu”.

Mtibwa imetoka kufungwa na Stand United 2-1, kisha ikafungwa na Mwadui FC 3-1, kabla ya kutoka suluhu na Mbao FC Jumapili iliyopita.

PSG yamtia hofu Ronaldo
Unga kwenye bahasha wampeleka mke wa Trump Jr hospitali