Waziri wa Maliasili na Utalii Dkt. Hamisi Kigwangalla amewataka wanaosema anakurupuka waseme uamuzi gani ameufanya kwa kukurupuka ili aweze kutoa maelezo na sio kumhukumu bila kumsikiliza.

“Mimi najitoa kupigania maliasili zetu natukanwa na kushambuliwa. Hiyo ndiyo shukrani stahiki? Tembo walikuwa 130,000 mwaka 2008, mwaka 2014 walibaki 8000! na mauaji haya wapo, na tunawajua Waziri akijitoa kuwashughulikia , amekurupuka!” amesema Kigwangalla

Kigwangalla anatuhumiwa na wabunge na kamati ya kudumu ya Bunge la Ardhi kuhusiana na uamuzi aliochukua wa kufuta leseni zote za umiliki wa vitalu kwa mwaka 2018-2022, leseni zilizotolewa kihalali na wizara.

Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa (Chadema) amesikika akisema anamshangaa Kigwangalla kwa hatua hiyo na kwamba anafanya kazi kwa mihemko.

Kufuatia tuhuma hizo Kigwangalla ametumia ukurasa wake wa ‘Twitter’ kuandika baadhi ya ujumbe uliashiria kujibu hoja hizo zinazomkabili.

“Haya maneno yanajirudia sana. Hebu nisaidie maeneo mawili tu ambapo unahisi ‘nimekurupuka ‘ ama ‘mihemko’ ili nitoe ufafanuzi. Maana mnafuata maneno ya mashambulizi ya watu wenye maslahi yaliyokanyagwa na mabadiliko tunayofanya kuliko kutazama ukweli kwa uhalisia wake” ameandika Kigwangalla.

Hayo yameandikwa na Kigwangalla akijaribu kujibu baadhi ya tuhuma alizoshambuliwa nazo akiwa Bungeni akijibu hoja.

Selembe aendelea kulikoroga Majimaji FC
Burundi yapingana na takwimu za UNHCR