Mwanafamilia wa kundi la Nako 2 Nako na mwanahisa wa kampuni ya Weusi inayozalisha muziki mzuri, G- Nako amesema kuwa mkumbo wa wasanii kufanya matukio yasiyo na tija kwa lengo la kujipatia ‘kiki’, ni moja kati ya mambo yanayomkata (yanayomkera) sana.

Akizungumza leo kwenye The Playlist ya Times Fm, G – Nako amesema kuwa wasanii wanaofanya matukio hayo ndio wanaorudisha nyuma muziki wa kizazi kipya na kuwafanya hata watu wenye heshima walikuwa wanaukubali, kuanza kuuona tena kama muziki wa kihuni.

G- Warawara ametumia maneno makali dhidi ya watu hao akidai wanachokifanya ni pumbavu na kuharibu muziki kwa kufanya yasiyohusika kwenye sekta hiyo.

“Umekuja hapa fanya kilichokuleta, fanya muziki mzuri na sio huo upumbavu. Kwakweli hili suala la kiki mimi linanikata sana, yaani linanikata na nina hasira sana na hao wanaofanya upumbavu,” alisema G-Nako.

Alisema wanachokifanya Weusi na hasa yeye ni kuhakikisha wanafanya muziki mzuri unaojiuza kwa mashabiki na sio kutengeneza matukio ya ‘kipumbavu’ kwa lengo la kutengeneza gumzo mitandaoni.

G Nako ni moja kati ya wasanii wachache ambao ukifuatilia kipaji cha muziki wake ni kama kuwa ndani ya duka kubwa (Supermarket) lenye kila unachokihitaji na zaidi.

Miaka miwili iliyopita, mashabiki na wasanii wenzake walimpa taji la kuwa mkali wa kufanya viitikio na ‘kuua’ kwenye mashairi. Mmoja kati ya waliompigia saluti G-Nako kwenye vyombo vya habari ni Mwana FA.

 

Cuba yapata rais mpya, familia ya Castro yang'atuka
Diamond, Nandy wajuta... TCRA yawaonesha njia