Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF) limetangaza kikosi cha timu ya Taifa ya Vijana wenye umri chini ya miaka 13 (U13) kitakacho kuwa jijini Mwanza kujiandaa na fainali za Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 17 mwaka 2019 nchini Tanzania.

Mapema mwezi Juni mwaka huu TFF iliandaa mashidano ya Taifa ya vijana yaliyofanyika jijini Mwanza ambapo japo la makocha chini ya Idara ya ufundi ya TFF, waliweza kuchagua vijana wenye vipaji ambao wanaunda timu hiyo.

Vijana hao wenye vipaji watakua wakiishi, kufundishwa mpira na kusoma katika shule ya Alliance iliyopo jijini Mwanza ambayo TFF imeingia mkataba na shule hiyo kwa ajili ya kuwalea wachezaji hao na kuendeleza vipaji vyao.

Mpango huo wa kuandaa kikosi cha vijana utafanyika pia mwakani kwa kuchagua vijana wenye umri chini ya miaka 14 (U14), na mwaka unaofuata kwa vijana wenye umri chini ya miaka 15 (U15) kwa lengo la kuendelea kuboresha kikosi hicho cha vijana.

Wachezaji waliochaguliwa kujiunga na timu hiyo ya vijana ni  Jaffar Juma (Arusha), Moris Michael (Ilala – Dsm), Jonathan Raphael (Kasulu – Kigoma), Karim Mfaume (Lindi), Erick Buyaga (Nyamagana – Mwanza), Shabani Kimwaga (Kinondoni – Dsm), Feisally Awadh (Ilala – Dsm), Abdulatif Noor (Tanga), Edmond Godfrey (Geita) na Adam Selemani (Kibaha – Pwani).

Wengine ni Selaman Juma (Kibaha – Pwani), Wilbert John (Ilala – Dsm), Ahsante Hamisi (Kinondoni – Dsm), Isaya Ernest (Mbeya), Gasper Gombanila (Nyamagana – Mwanza), Joseph Awadh (Ilala – Dsm), Alfonsi Mabula (Nyamagana  – Dsm), Cosmas Lucas (Nyamagana – Mwanza), Haroub Juma (Bariadi – Simiyu) na Ladak Juma (Morogoro).

Wakati huo huo wachezaji watano kutoka kikosi cha timu ya Taifa cha vijana wenye umri chini ya miaka 15 (U15) wanatarajiwa kuondoka nchini mwishoni mwa mwezi huu wa Agosti kuelekea nchini Afrika Kusini kwa ajili ya majaribio katika klabu ya vijana ya Orlando Pirates.

Nafasi hiyo imepatikana kufuatia mazungumzo ya Rais wa TFF, Jamal Malinzi na Rais wa klabu hiyo Irvin Khoza kuomba vijana hao kupata nafasi ya kufanya majaribio katika klabu hiyo na endapo watafuzu, watajiunga na timu ya vijana ya Orlando Pirates.

Wachezaji hao ni Asaad Ali Juma (Zanzibar), Maziku Amaan (Dodoma), Issa Abdi (Dodoma), Kelvin Deogratias (Geita) na Athumani Maulid (Kigoma) wataongozana na Mkurugenzi wa Ufundi wa TFF, Salum Madadi kuelekea Afrika Kusini Agosti 28, 2015 kwa ajiliya kufanya majaribio hayo.

Figisu Figisu Za Usajili Ulaya
NEC Yazungumzia Tuhuma Za Kutumia Wanajeshi