Rais mstaafu, Jakaya Kikwete amempa nasaha  za maisha ya ndoa na ujana, Ali Kiba ambaye yuko kwenye harakati za kufunga ndoa hivi karibuni.

Ingawa taarifa za awali kutoka Mombasa zimekuwa zikieleza kuwa mwanamuziki huyo tayari ameshafunga ndoa na mrembo Aminah Rekish wa eneo hilo la mwambao, ujumbe wa rais mstaafu unatupatia mwanga zaidi kuwa tukio rasmi litafanyika hivi karibuni.

Ali Kiba amemtembelea rais huyo mstaafu nyumbani kwake. Hakutoka mikono mitupu, bila shaka ameongezewa busara zaidi za maisha.

Kupitia twitter, Kikwete ameweka picha inayomuonesha akiwa na Ali Kiba pamoja na mwanafamilia mwenzake wa RockStar 4000, Ommy Dimpoz katika picha ya pamoja iliyomjumuisha pia mama Salma Kikwete.

“Namshukuru @officialalikiba kuja kunitembelea na kunitaarifu kuwa anatarajia kuoa hivi karibuni. Nimempatia nasaha zangu na namtakia kila lakheri kwa jambo hilo jema aliloamua kufanya,” Kikwete ameandika.

Aprili 19, inatajwa kuwa siku ambayo King Kiba atakula kiapo cha kuishi kwenye raha na shida na malkia wake Aminah, mtoto wa mwambao wa Mombasa nchini Kenya.

Ali Kiba anakuwa msanii wa pili mkongwe wa bongo fleva kuvuka mipaka kufunga pingu za maisha baada ya AY kufanya hivyo katika wiki ya kwanza ya Februari, akivuta kifaa kutoka Rwanda.

 

Ali Kiba afunga ndoa rasmi, mama mkwe afunguka yaliyojiri
Trump apongeza mashambulizi ya kijeshi Syria, Putin atoa onyo kali