Imeelezwa kuwa Kilimo kinachotumia teknolojia ya kisasa ya umwagiliaji ndiyo njia sahihi ya utatuzi wa changamoto zitokanazo na mabadiliko ya tabianchi katika sekta ya kilimo.

Hayo yamesemwa jijini Dar es Salaam na Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Uendelezaji wa Teknolojia ya Umwagiliaji, Anthony Nyarubamba kutoka Tume ya Taifa ya Umwagiliaji, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake.

Amesema kuwa Kilimo hicho cha Umwagiliaji kinatumia teknolojia ya kisasa ya njia ya matone ya maji pamoja na kuvuna maji ya mvua katika mabwawa maalum, yaliyojengwa katika maeneo ya mashamba ya umwagiliaji.   

Aidha, Nyarubamba amesema kuwa uvunaji huo wa maji ya mvua unapelekea kuzuia mafuriko mengi yanayosabishwa na kubadilika kwa hali ya hewa kunakoharibu kwa kiasi kikubwa miundombinu mingine kama vile madaraja na barabara.

“Serikali iongeze rasilimali za kutosha katika kilimo cha umwagiliji, ili kuweza kujenga mabwawa ya kutosha kupokea maji katika maeneo yenye skimu za umwagiliaji na kupunguza athari zitokanazo na mabadiliko ya tabianchi,”amesema Nyarubamba

Hata hivyo, ameongeza kuwa kuwa skimu nyingi zilizopo katika kanda zote nane za Mbeya, Mtwara, Morogoro, Kilimanjaro, Dodoma, Tabora Katavi na Mwanza, zimefanikiwa kwa kiasi kikubwa na kuongeza Uzalishaji, Ajira na  Kipato kwa vijana wengi, hasa kutokana na ukulima wa vitunguu katika kanda ya Mbeya na Mpunga katika kanda ya Kilimanjaro.

 

 

Makonda atumia mamilioni kuwakatia Bima ya Afya watoto yatima
Wanasaikolojia wabaini hili katika mahusiano na uchepukaji njia kuu