Ukifuatilia maisha ya sasa ya Mwanamitindo Kim Kardashian utagundua mambo yameanza kumbadilikia na licha ya mengi yaliyojitokeza, kwa sasa unaweza ukawa wakati wake kumkumbuka aliyekuwa mume wake rapa Kanye West, utajiuliza kwanini?

Hii ni kutokana na mwenendo mzima wa maendeleo yake kwenye upande wa ubunifu na mitindo ambao muda mfupi baada ya kutalikiana na Kanye, ubora na viwango vyake vya juu vimeonekana kuporomoka na kupoteza mvuto.

Imetajwa tofauti na alivyokuwa hapo awali ambapo ubunifu, umahiri na mvuto wa hali ya juu ulikuwa ni moja ya sifa kuu za mrembo huyo maarufu duniani.

Inaelezwa kuwa rapa Kanye West alikuwa akihusika kwa kiwango kikubwa kuutegeneza muonekano wa Kim hasa anapotokea mbele ya hadhira kwenye matukio mbali mbali ‘Red carpet’, mrembo huyo alionekana kuwa malkia wa siku kutokana na muonekano pamoja na mpangilio wa mitindo ya mavazi.

Katika kipindi chake kipya cha luninga Kim alidhihirisha hilo akimwambia Kourtney Kardashian, kwamba kwa namna fulani kutokana na imani aliyokuwa nayo kwa Kanye kuhusu ubunifu na uwezo mkubwa wa kufahamu mitindo ilifika pahala yeye ndio alikuwa kila kitu kwenye upande huo..

“Nilifika mahali ilikuwa nikimuomba ushauri kwenye kila kitu, hadi kile ninachovaa. Hata sasa mara nyingi ninapatwa na hofu inapofikia ninawaza, ‘Ninavaa nini?” amesema Kim.

Amebainisha kuwa hata vazi lake alilovaa kwenye hafla ya Wall Street Journal Magazine Innovator Awards, hakuwa na uhakika nalo, kutokana na kuukosa ushauri wa Ye, ambaye muda wote alimfanya mrembo huyo kuonekana vyema.

“Nilikuwa kama, najishtukia huku nikiwaza ‘Ninavaaje kitu ambacho hakijachunguzwa kwanza?” aliongeza Kim.

Kim anabainisha wazi kuwa Kanye hakuwa shabiki mkubwa wa chochote alichokuwa akichagua mrembo huyo na hata kuamua kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha mke wake anapendeza kupitia yeye na muda mwingi alimdhihaki kwa utani.

Mpenzi wa kwanza wa Kanye baada ya kuachana na Kim, ni mwigizaji Julia Fox ambaye pia alijikuta akibadilika kwa kiasi kubwa kwenye upande wa mavazi na namna alivyokuwa akitokea kwenye matukio/hafla mbali mbali.

Hili suala la mitindo pekee linaweza kumfanya Kim ajutie kuachana na Kanye?, tupige kwanza mtori nyama tutazikuta chini.

Sasa kwa kuwa wakati huu Kanye yuko kwenye uhusiano wa kimapenzi na mwanamke mwingine, Mrembo Chaney Jones ambaye kwa kiasi kikubwa ana mfanano na Kim, pengine tunaweza kuona tofauti katika mtindo wake, maana kwa kiasi kikubwa anavaa kama Kim.

Kanye anapachikwa cheo cha ziada na wadau wa mitindo wakimwita mwanaume ambaye kwa hakika huwafanya wanawake wake kuwa jumba lake la kumbukumbu na ubunifu mitindo.

Wanawake wana akili na nguvu zaidi kuliko sisi wanaume - Majid Michel
Habari kuu kwenye Magazeti ya leo Mei 14, 2022