Mchambuzi wa soka la nchini Hispania Guillem Balague amewanyima nafasi mameneja wa klabu za Liverpool na Arsenal Jurgen Klopp na Arsene Wenger ya kuwa wakuu wa benchi la ufundi la FC Barcelona endapo wataamua kuachana na Luis Enruique mwishoni mwa msimu huu.

Mara kadhaa taarifa zinaeleza kuwa, FC Barcelona wanafikiria kubadili benchi lao la ufundi na baadhi ya watu wanaofikiria yupo meneja wa sasa wa Liverpool na Arsenal.

Rais wa FC Barcelona Josep Maria Bartomeu mwezi Aprili atakutana na jopo la viongozi wengine klabuni hapo kwa ajili ya kusaka njia mbadala ya kuliboresha benchi lao la ufundi, ama kumuajiri mtu mwingine ambaye atakwenda na wasaidizi wake.

“FC Barcelona hawawezi kufanya kazi na Klopp ama Wenger,” Balague aliiambia Sky Sports.

“Hata kama Klopp anaonyesha huenda akawa sehemu ya wanaofikiriwa kwenye orodha ya mameneja, lakini ninakuhakikishia haiwezekani akakabidhiwa jukumu la kukiongoza kikosi cha FC Barceklona, Hali kadhali kwa Wenger, jambo hilo haliwezi kutokea kamwe.”

Hata hivyo Balague ameonyesha kuwa na imani kubwa ya kumuona meneja wa sasa wa klabu ya Sevilla Jorge Sampaoli akikabidhiwa jukumu la kukinoa kikosi cha FC Barcelona kuanzia msimu ujao, kutokana na uwelewa wa soka la nchini Hispania alionao.

Wengine wanaodhaniwa na mchambuzi huyo ni meneja wa klabu ya Athletic Bilbao Ernesto Valverde, Mauricio Pochettino wa Tottenham Hotspur, Eusebio Sacristan wa Real Sociedad na  Ronald Koeman wa Everton.

Mchungaji aambulia kichapo kanisani
NHC kumaliza kero za makazi ya nyumba kwa Watanzani